Connect with us

News

Viongozi wa dini Kanda ya Kati wataka amani uchaguzi mkuu

Published

on

Na Mwandishi Wetu, Dodoma

VIONGOZI wa dini mbalimbali kutoka Kanda ya Kati wamewataka Watanzania kuendelea kulinda amani ya nchi na kujitokeza kwa wingi kushiriki katika Uchaguzi Mkuu unaotarajiwa kufanyika Oktoba 29, 2025, wakisisitiza kuwa amani ni tunu na urithi wa thamani unaopaswa kulindwa na kila raia.

Wito huo umetolewa leo Oktoba 25, 2025, katika Kongamano la Amani lililofanyika jijini Dodoma, likijumuisha viongozi wa dini kutoka mikoa ya Dodoma na Singida.

Katika kongamano hilo, viongozi hao walijadili mada mbalimbali kuhusu umuhimu wa kupiga kura, historia ya chaguzi nchini na wajibu wa kila raia kulingana na Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Akitoa mada kuhusu umuhimu wa amani, Mwenyekiti wa Baraza la Makanisa ya Kikristo Tanzania (CCT) Mkoa wa Dodoma na Askofu wa Kanisa la Mennonite Tanzania (KMT), Joseph Mtolela, amesema Tanzania imeendelea kuwa kisiwa cha amani katika kipindi chote cha kampeni, na hivyo ni jukumu la kila mmoja kuhakikisha hali hiyo inaendelea hadi baada ya uchaguzi.

“Siku nne zijazo nchi yetu itakuwa kwenye mchakato wa uchaguzi. Tumekuwa na amani katika kipindi chote cha kampeni, na tunahitaji amani hiyo siku ya uchaguzi. Tushiriki kwa wingi, tuwe makini kuangalia chama au kiongozi atakayeleta amani, utulivu na usalama wa nchi,” amesema Askofu Mtolela.

Ameongeza kuwa amani ni zawadi kutoka kwa Mungu na ndiyo msingi wa maendeleo ya taifa.

“Mungu ameturuzuku amani, ni kipaji na kipawa. Tuna kila sababu ya kuitunza na kuilinda, kwani bila amani hakuna maendeleo, wananchi hawatakuwa salama, na tutakimbia nchi yetu wenyewe,” amesisitiza.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Jumuiya ya Maridhiano Mkoa wa Dodoma, Askofu Evance Chande wa Kanisa la Karmel Assemblies of God, amesema moyo wa uzalendo miongoni mwa Watanzania umeanza kupungua, na kuwataka viongozi wa dini kuungana kuhakikisha nchi inabaki salama.

“Sisi viongozi wa dini tuna jukumu kubwa kuhakikisha tunasimama kwenye nafasi zetu. Adui anapambana kuondoa amani, hivyo lazima tuamke, tushirikiane na Serikali, tuelimishane na hasa vijana wetu ambao mara nyingi hutumiwa vibaya. Tuwape elimu ya uzalendo na kuwaonya kutokuitumbukiza nchi kwenye migogoro,” amesema Askofu Chande.

Kwa upande wake, Sheikh wa Mkoa wa Singida, Issa Nassoro, amesema jukumu la kulinda amani liko mikononi mwa viongozi wa dini na waumini wao.

“Tatizo si sisi viongozi, bali baadhi ya waumini wetu wanaopoteza hofu ya Mungu na kuwa chanzo cha uvunjifu wa amani. Tunapaswa kurudi kwao, kuwaonya na kuwaelimisha. Mwanzo wa moto ni cheche; tusiruhusu cheche hiyo iwake,” amesema Sheikh Nassoro.

Amesisitiza kuwa kushiriki uchaguzi ni sehemu ya kulinda amani. “Amani ni bora kuliko riziki. Jamii yoyote isiyoshiriki kupiga kura inajinyima haki ya kupata viongozi wanaokubalika, na matokeo yake ni vurugu. Ni jukumu letu kuwahamasisha watu kupiga kura kwa amani na kuchagua viongozi wenye maono ya kulinda mema ya taifa,” amesema Sheikh Nassoro.

Naye Askofu Zephania Mkuyu wa Kanisa la Tanzania Assemblies of God (TAG) Dodoma Magharibi, amesema suala la amani halina uhusiano wa kisiasa bali ni la kiroho, hivyo viongozi wa dini wanapaswa kuendelea kuhubiri amani na kuombea nchi.

“Kama viongozi wa dini tutasimama katika nafasi zetu, tutaona matokeo mazuri. Amani ni nguzo ya maendeleo ya kiroho, kijamii na kiuchumi,” amesema Askofu Mkuyu.

Kwa upande wake, Sheikh wa Mkoa wa Dodoma, Alhaji Dkt. Mustapha Rajabu, amesema raia wote wanapaswa kuwa watiifu kwa viongozi wa dini na Serikali, na kuzingatia maelekezo yao kuhusu uchaguzi.

“Maandamano halali ni kwenda kupiga kura. Tarehe 29 wajitokeze kwa wingi, wachague viongozi watakaoliletea taifa maendeleo. Bila amani, familia zitaathirika na miundombinu kuharibika,” amesema Sheikh Rajabu.

Aidha, Mshauri wa Mufti, Alhaji Ismail Dawood, amewataka wananchi kutokuwa na hofu bali kujitokeza kupiga kura kwa amani, akisema:
“Tusihofu vurugu, twendeni tukapige kura. Naomba waumini wote wakusanyike tarehe 29 kwenda kupiga kura kwa utulivu.”

Kongamano hilo lilihitimishwa kwa wito wa pamoja kutoka kwa viongozi wa dini wote waliohudhuria, wakiahidi kuendelea kuelimisha waumini wao kuhusu kulinda amani, kudumisha umoja wa kitaifa na kushiriki uchaguzi kwa amani na utulivu.

Continue Reading
Click to comment
0 0 votes
Article Rating
Subscribe
Notify of
guest
0 Comments
Oldest
Newest Most Voted
Inline Feedbacks
View all comments

News

Wanawake 142 waanza mafunzo ya Female Future Programme Dar es Salaam

Published

on

By

Na Mwandishi wetu, News info

Zaidi ya wanawake 142 wamepokelewa rasmi kushiriki toleo la 12 la programu ya mafunzo ya uongozi kwa wanawake, Female Future Programme (FFP), iliyofanyika jijini Dar es Salaam.

Mafunzo hayo ya kiutendaji yameandaliwa na Chama cha Waajiri Tanzania (ATE) kwa kushirikiana na Taasisi ya Usimamizi ya Afrika Mashariki na Kusini (ESAMI).

Mkurugenzi Mtendaji wa ATE, Bi. Suzanne Ndomba-Doran amesema programu hiyo imekuwa na mchango mkubwa kwa zaidi ya wanawake 800 waliokwisha pata mafunzo kwa zaidi ya muongo mmoja, na sasa inaendeshwa katika nchi sita kwa ufadhili wa NHO, huku akiwahamasisha washiriki kushiriki kikamilifu safari ya miezi tisa ya mafunzo. Aidha, Naibu Mkurugenzi Mkuu wa ESAMI, Dkt. David Kalaba amesema jamii inahitaji wanawake viongozi wenye kujiamini na uwezo mkubwa katika kipindi hiki cha mabadiliko ya haraka, akisisitiza umuhimu wa mtazamo wa kimataifa, kujifunza na kuendana na mabadiliko pamoja na uwezo wa kusimamia utofauti, kutatua migogoro na kutoa thamani kwa wateja.

Kwa upande wake, Meneja wa Upstream wa IFC, Bw. Sam Nganga aliyemwakilisha Meneja wa Nchi, Bi. Martine Valcin amesema taasisi hiyo inaendelea kuhakikisha wanawake wanapewa nafasi katika ngazi za juu za uongozi ili kukuza ushirikishwaji, huku akiwahimiza washiriki kujisimamia na kutumia kikamilifu mafunzo hayo.

Katika hafla hiyo pia kulikuwa na mjadala wa jopo kuhusu wanawake katika uongozi uliowashirikisha wataalamu mbalimbali wa rasilimali watu na uongozi kutoka taasisi tofauti, ambapo ilisisitizwa kuwa kuchanganya uzoefu wa vizazi tofauti vya wanawake kazini huleta matokeo chanya pamoja na umuhimu wa kujifunza ujuzi mpya na kuimarisha mentorship baada ya mafunzo.

Washiriki wa kundi la 12 walihimizwa kujenga mitandao imara ya kitaaluma, huku taasisi na makampuni yakitakiwa kutambua upekee wa kila mwanamke badala ya kuwaona kama kundi moja.

Akihitimisha, Mjumbe wa Bodi ya ATE, Bw. Gasper Kikui amesema sekta isiyo rasmi bado ina changamoto nyingi za uongozi na kuwataka washiriki kuyachukulia mafunzo hayo kwa uzito ili kuleta mabadiliko chanya.

Continue Reading

News

Dkt Samia: Vijana wanufaike na uwekezaji katika mawasiliano

Published

on

By

Na Mwandishi wetu, News info

Rais Dkt Samia Suluhu Hassan, ametaka vijana wanufaike ipasavyo na huduma za mkongo wa Taifa wa mawasiliano, hasa katika maeneo ya kukuza ubunifu, ujuzi wa kidigitali na fursa za ajira.

Ametaka Wizara ya Mawasiliano na Teknolojia ya Habari na Wizara ya Nchi, Ofisi ya Rais, Maendeleo ya Vijana, zishirikiane na wadau wa sekta ya teknolojia ili vijana wapate manufaa hayo.

Dkt Samia ameyasema hayo leo, Ijumaa Aprili 10, 2026 jijini Dodoma, wakati wa uzinduzi huo, ukiambatana na kuunganisha huduma za mkongo wa Taifa wa mawasiliano katika Wilaya 85.

“Uwekezaji huu kwa vijana ni muhimu kwa sababu dunia ya teknolojia ni ya kwao. Dunia hii ipo viganjani mwao na ndiyo mfumo wa maisha yao. Ni lazima tuwawezeshe na kuwahamasisha kutumia mifumo hii ili waweze kukua kiuchumi na kijamii,” amesema.

Continue Reading

News

Dkt Samia azindua minara 758, kuwanufaisha zaidi ya wananchi milioni nane

Published

on

By

Na Mwandishi wetu, News info

Zaidi ya wananchi milioni 8.5 hususan wanaoishi mipakani na vijijini, wanatarajiwa kuondolewa changamoto ya mtandao, baada ya Rais Dkt Samia Suluhu Hassan, kuzindua minara 758 ya mawasiliano iliyojengwa katika maeneo mbalimbali nchini.

Uzinduzi huo umefanyika leo Ijumaa Aprili 10, 2026 jijini Dodoma, ukiambatana na kuunganisha huduma za mkongo wa Taifa wa mawasiliano katika Wilaya 85, ikiwa ni juhudi za Serikali kuimarisha uchumi wa kidijitali na kuongeza huduma za mawasiliano.

Akizungumza wakati wa uzinduzi huo, Dkt Samia amesema uwekezaji huo umetokana na ushirikiano kati ya Serikali na wadau wa sekta ya mawasiliano ili kuhakikisha huduma za mawasiliano zinawafikia wananchi kwa ubora unaokidhi mahitaji ya teknolojia ya kisasa na kwa gharama nafuu.

Amesema kukamilika kwa ujenzi wa minara hiyo kutachochea ushiriki wa wananchi katika uchumi wa kidijitali na kufungua fursa mpya za ajira, kuboresha utoaji wa huduma za kijamii na kuharakisha maendeleo ya Taifa.

“Mawasiliano si tena huduma ya anasa kama ilivyokuwa zamani. Leo hii ni uti wa mgongo wa uchumi wa kisasa na daraja la fursa kwa wananchi katika nyanja mbalimbali za maendeleo,” amesema

Continue Reading

Trending

Copyright © 2025 Newsinfo.