Uncategorized
NMB Foundation yawanoa Wakulima wa Zao la Kakao Kyela, Serikali yaipongeza
News
Mradi wa TAZA kufungua soko jipya la biashara ya umeme afrika.
Na Mwandishi Wetu, Mbeya
Imeelezwa kuwa mradi wa ujenzi wa njia ya kusafirisha umeme ya msongo wa kilovoti 400 kutoka Iringa hadi Zambia kupitia Tunduma (TAZA) umefikia asilimia 83.45 huku ukitarajiwa kukamilika ifikapo Mei 2026 na hivyo kufungua soko jipya la biashara ya umeme barani Afrika.
Akizungumza wakati wa ziara ya kukagua utekelezaji wa mradi huo leo Oktoba 23, 2025 katika eneo la Iganjo, Mbeya, Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Nishati, Dkt. James Mataragio amesema mradi wa TAZA ni muhimu kwa Taifa kwa kuwa utaiunganisha Tanzania na Nchi za ukanda wa Kusini mwa Afrika (Southern Africa Power Pool) na pia kuimarisha muunganiko wa ukanda wa Mashariki mwa Afrika (East Africa Power Pool).
“Nimshukuru na kumpongeza Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kutenga fedha kwa ajili ya utekelezaji wa miradi mikubwa ya nishati. Kupitia mradi huu tutaimarisha biashara ya kuuza na kununua umeme kati ya nchi za Mashariki mwa Afrika na zile zilizopo Kusini mwa Afrika”. Amesema Dkt. Mataragio
Kuhusu biashara ya umeme ya kikanda, Dkt. Mataragio amesema kuwa tayari Tanzania imeshaunganisha gridi ya umeme na Nchi za Afrika za Kenya, Rwanda, Burundi na Ethiopia kupitia muunganiko wa East Africa Power Pool.
“Tutaunganisha pia gridi na nchi za Kaskazini na Magharibi mwa Afrika ili Afrika nzima tuweze kuuziana umeme ikiwa ni sehemu pia ya kutekeleza Mpango wa Nishati unaolenga kuwafikishia umeme waafrika takribani milioni 600 ambao bado hawajafikiwa na nishati ya umeme”. Amesisitiza Dkt. Mataragio.
Kuhusu mradi wa TAZA, ameeleza kuwa unatekelezwa na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kushirikiana na wadau wa maendeleo ambao ni Benki ya Dunia, Umoja wa Ulaya na Shirika la Maendeleo la Ufaransa kwa Dola za kimarekani milioni 584.
Amesema kuwa mbali ya mradi wa TAZA kuunganisha gridi za umeme za Nchi za Kusini mwa Afrika, utauunganisha Mkoa wa Rukwa na umeme wa gridi pamoja na kuboresha hali ya upatikanaji wa umeme katika Mikoa ya Iringa, Njombe, Mbeya na Songwe.
Baada ya kukagua mradi huo, Dkt. Mataragio ameliagiza Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) kuhakikisha linamsimamia Mkandarasi kwa karibu hasa katika kipindi hiki cha mvua ili hatua za awali za ujenzi wa misingi (foundation) ziweze kukamilika kwa wakati na kumtaka Mkandarasi kuhakikisha vifaa vyote vipo eneo la Mradi.
Katika hatua nyingine Dkt. Mataragio ameiagiza TANESCO kuhakikisha inapeleka umeme eneo la Ngozi unapotekelezwa mradi wa kuzalisha umeme kwa jotoardhi ambapo kwa hivi sasa mitambo ya uhakiki wa jotoardhi katika eneo hilo inatumia mafuta ya dizeli.
Katika ziara hiyo Naibu Katibu Mkuu aliambatana na Kamishna wa Umeme na Nishati Jadidifu Mha. Innocent Luoga na watendaji wa Wizara ya Nishati na TANESCO.










News
Viongozi wa dini Kaskazini wahimiza amani kuelekea Uchaguzi Mkuu
Na Mwandishi wetu, Newsinfo Online
VIONGOZI wa dini kutoka mikoa ya kanda ya kaskazini, wamewataka Watanzania kulinda amani ya nchi, hasa taifa linapoelekea katika Uchaguzi Mkuu, wakisisitiza kuwa amani ni nguzo muhimu kwa ustawi wa taifa.
Viongozi hao kutoka mikoa ya Tanga, Arusha, Manyara na Kilimanjaro wametoa kauli hiyo leo Oktoba 22, 2025 katika Kongamano la Amani na Uchaguzi lililofanyika mjini Moshi.
Mwishoni mwa kongamano hilo lililoongozwa na kauli mbiu ‘Kupiga kura ni haki yetu na amani ya nchi yetu ni wajibu wetu’, viongozi wa Dini wamesoma maazimio, yanayosisitiza ulinzi wa amani ya nchi na kuhimiza wananchi kushiriki katika uchahuzi mkuu wa Oktoba 29, 2025.
Akisoma maazimio hayo, Katibu wa BAKWATA Wilaya ya Moshi, Alhaji Awadhi Lema ametaja mambo saba yaliyokubaliwa na viongozi wa dini kuwa ni pamoja na kuhamasisha wananchi waliojiandikisha kuhakiki majina yao na kujitokeza kupiga kura.
Azimio jingine ni kuwataka Watanzania kuepuka uchochezi kupitia mitandao ya kijamii na vyombo vya habari, Vyombo vya dola kutumia hekima na busara kulinda amani siku ya uchaguzi, kupanua ushiriki wa viongozi wa dini katika vyombo vya maamuzi na utungaji wa sheria pamoja na kila mwananchi kuwa na wajibu wa kulinda amani wakati wa kudai haki yake.
Akizungumza katika Kongamano hilo, Sheikh wa Mkoa wa Kilimanjaro, Mlewa Shaban, amesema hakuna amani ya kweli bila haki, usalama wa uhai na mali.
Amefafanua kuwa, jukumu la kulinda amani si la serikali pekee bali ni la kila raia, akisisitiza umuhimu wa kuepuka chuki, uongo na maneno ya kuchochea mgawanyiko.
“Kuua mtu mmoja ni sawa na kuondoa amani kwa jamii nzima na raia mwema ni yule anayejenga amani kwa wengine. Amani hujengwa kwa uvumilivu, uadilifu na kuheshimiana bila kujali tofauti za kidini, kikabila au kisiasa,” amesema Sheikh Mlewa.
Mwanasheria wa KKKT Dayosisi ya Kaskazini, Mch. Wakili Daniel Swai aliyemwakilisha Askofu Fredrick Shoo, amesema amani na haki haviwezi kutenganishwa, kwani vinashikamana katika kujenga jamii yenye heshima na mshikamano.
Naye Padri Steven Msami kutoka Kanisa la Anglikana Tanga amesema amani ni tunda takatifu, na palipo na amani watu hukaa kwa utulivu.
“Tusiseme amani tu, bali tuseme na uvumilivu, kwani bila uvumilivu hakuna amani,” amesema.
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Umoja wa Vijana wa KKKT Dayosisi ya Kaskazini, Elinawinga Mariki amewataka wananchi kujitokeza kujiandikisha na kushiriki uchaguzi ili kupata viongozi wenye hekima na busara.
Katibu wa Bakwata, Mkoa wa Arusha, Ally Athuman Nassoro, amesisitiza kuwa amani haina mbadala, hivyo Watanzania wanapaswa kuilinda kila wakati wanapokutana na changamoto.
“Tumuombe Mungu atupe uongozi utakaoleta maisha bora kwa Watanzania,” amesema.
Yakoba Hassan, ambaye ni Mwenyekiti wa Jumuiya ya Kinamama Waislamu Moshi, aliomba vyombo vya ulinzi na usalama kuepuka kutumia nguvu kupita kiasi wakati wa uchaguzi, ili kudumisha amani iliyopo.
Awali akifungua kongamano hilo kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro, Nurdin Babu, Mkuu wa Wilaya ya Moshi, Godfrey Mzava, amesema Tanzania inaelekea kwenye uchaguzi wa kikatiba na kidemokrasia huku hali ya amani ikiendelea kutawala mkoani humo.
“Tunaendelea kuwasihi wananchi kujitokeza kwa wingi siku ya kupiga kura kwa sababu ni haki yao ya msingi. Serikali itahakikisha usalama na haki vinatawala katika mchakato mzima wa uchaguzi,” alisema Mzava.
Aliongeza kuwa serikali inafarijika kuona viongozi wa dini wanashirikiana katika kulinda amani, kwani maoni na ushauri wao ni mchango muhimu kwa serikali na jamii.








Uncategorized
NMB Yaandika Historia kwa Kushinda Tuzo Sita Kubwa, Ikiwemo ya “Benki Bora kwa Uendelevu Barani Afrika”

Dar es Salaam
Benki ya NMB inatangaza mafanikio ya kihistoria ya ushindi wa tuzo sita za kimataifa kutoka kwa majarida mawili mashuhuri duniani – jarida la Euromoney linalochapishwa London, Uingereza, na Global Banking & Finance Magazine lenye makao makuu yake New Jersey, Marekani.
Ushindi huu mkubwa unaashiria kutambuliwa kwa ubora wa huduma, ubunifu na mchango wa Benki ya NMB katika kuchangia maendeleo endelevu ya kiuchumi nchini.
Miongoni mwa tuzo hizo ni ile ya heshima ya “Benki Bora kwa Uendelevu Barani Afrika” inayodhibitisha mafanikio na maendeleo makubwa ya NMB na tasnia nzima ya fedha nchini.
Tuzo ya “Benki Bora kwa Uendelevu Barani Afrika”, iliyotolewa hivi karibuni jijini London katika hafla ya Euromoney Private Banking Awards 2025, imeweka historia kwa kuwa ya kwanza kutolewa kwa Benki ya Kitanzania.. Hii ni hatua kubwa ya kutambua mchango wa Tanzania katika eneo nyeti la uendelevu, ambalo lina umuhimu mkubwa katika maendeleo ya kijamii, kiuchumi na mazingira duniani kote.



Ushindi huu unadhihirisha jitihada za Benki ya NMB za kuongoza mabadiliko na dhamira yake ya dhati za kuyafanya masuala ya mazingira, jamii na utawala bora (ESG) kuwa sehemu ya msingi katika shughuli zake za kiutendaji na dira yake ya kimkakati.
Benki ya NMB pia ilinyakua tuzo mbalimbali kama kinara wa kitaifa katika sekta ya benki kutoka kwa majarida hayo mawili kama ifuatavyo:
Euromoney:
● Benki Bora ya Uendelevu Tanzania
● Benki Bora ya Wateja Maalum Tanzania (kwa mwaka wa tatu mfululizo)
Global Banking and Finance Magazine:
● Benki Salama Zaidi Nchini Tanzania
● Kinara wa Uwajibikaji kwa Jamii Tanzania 2025
● Afisa Mtendaji Mkuu Bora wa Benki Tanzania 2025 (Tuzo hii ilitolewa kwa CEO Ruth Zaipuna)
Afisa Mtendaji Mkuu wa NMB, Bi Ruth Zaipuna alipongeza kwa tuzo hizo huku akisema : “Ni hatua ya kihistoria kwa tasnia ya fedha nchini. Aidha, alisisitiza kuwa tuzo hizi ni hatua muhimu katika kuisaidia Tanzania kujipambanua kama kiongozi wa kikanda wa ufadhili endelevu na utoaji wa huduma bora za kifedha.
“Ni heshima kubwa kwetu kutambuliwa na Euromoney na Global Banking & Finance Magazine kwa uongozi wetu katika Ufadhili Endelevu na Huduma kwa Wateja Maalum,” alisema Bi. Zaipuna. “Tuzo hizi sita ni ushahidi wa juhudi na kujitolea kwa wafanyakazi wetu,, imani kubwa ambayo wateja wetu wameendelea kutuonesha, na dhamira thabiti tuliyonayo ya kujenga mustakabali wa ustawi, ujumuishaji, na maendeleo endelevu kwa nchi yetu.”
“Sisi kama Benki ya NMB, uendelevu si tu ni wajibu wa kibiashara bali ni hitaji la kimkakati linalochangia uimara wa biashara, kuchochea ubunifu, kuongeza ushindani, na kuhakikisha upatikanaji wa thamani ya kudumu. Kwa kuufanya uendelevu kuwa kiini cha mkakati wetu wa biashara, tunawahakikishia wadau wetu thamani ya kudumu na kuwa na athari chanya kwa jamii tunazozihudumia.”
Benki ya NMB pia imepata heshima ya kutambuliwa kama Benki Salama Zaidi nchini Tanzania kutokana na dhamira yake thabiti katika maendeleo ya kiteknolojia na rasilimali watu.
“Tuzo hii ni matokeo ya moja kwa moja ya uwekezaji wa kimkakati katika ubunifu na hatua madhubuti za usalama wa mtandao, hali inayowezesha uwepo wa mazingira ambayo yanafanya wateja zaidi ya milioni 8.6 kuwa na imani na uimara wa kifedha wa Benki ya NMB na usalama wa fedha zao.
“Tumejidhatiti kukuza uwezo wetu na kuhakikisha ufanisi wa kifedha wa kudumu, tutaendelea kuwekeza katika teknolojia na rasilimali watu ili kukidhi mahitaji anuwai ya wateja wetu tunaowathamini kwa moyo wote,” alihitimisha Bi. Zaipuna.
Akizungumzia tuzo hizo, Mhariri Mkuu wa Euromoney, Bi. Louise Bowman, alisema, “Benki ya NMB imedhihirisha kuwa taasisi kinara wa maendeleo endelevu nchini Tanzania na barani Afrika kupitia mipango yake ya kimkakati inayozingatia uwiano wa uwajibikaji wa kimazingira, athari chanya kwa jamii, na ukuaji wa kifedha.”
Tuzo hizi zinabainisha dhamira ya Benki ya NMB katika uendelevu wa mazingira na jamii, sambamba na kutoa masuluhisho bora ya kifedha yenye viwango vya kimataifa, ambayo yanawawezesha wateja na kuchochea maendeleo jumuishi ya kiuchumi. Kutambuliwa huku ni uthibitisho wa maono ya kimkakati ya Benki ya NMB katika kuendeleza Ukuaji Jumuishi na Maendeleo Endelevu, huku ilipanua wigo wa upatikanaji wa huduma za kifedha kwa Watanzania wote.
Benki ya NMB inaendeleza kwa dhati dhamira yake ya kuzingatia viwango vya juu kabisa vya ubora wa huduma za kibenki, kuendeleza ubunifu, na kuchangia kikamilifu katika maendeleo endelevu ya Tanzania chini ya uongozi wa ushindi wa Bi. Zaipuna.
-
News8 months agoSABASABA AONGOZA CUSTOMER FORUM DODOMA
-
News11 months agoRais Samia apeleka Bilioni 669 za Barabara, Madaraja mikoa ya Kusini
-
Uncategorized11 months agoNMB Yaandika Historia kwa Kushinda Tuzo Sita Kubwa, Ikiwemo ya “Benki Bora kwa Uendelevu Barani Afrika”
-
News10 months agoFCC YATOA SEMINA YA MASUALA YA UHIBITI BANDIA KWA WAJASIRIAMALI WANAWAKE
-
News8 months agoTRA, NCAA, TANAPA na TAWA Kuunda Kamati Tendaji ya Pamoja Kuongeza Mapato
-
News10 months agoRais Mwinyi aizawadia Yanga Milioni 100
-
News11 months agoDkt. Biteko akutana na Mtendaji Mkuu wa PUMA Duniani
-
News4 months agoZaidi ya USD Milioni 9 uwekezaji mpya utafiti wa dhahabu Tanzania




