Connect with us

News

Makonda kuleta neema kwa vijana

Published

on

Na Mwandishi wetu, NewsInfo – Arusha

Mgombea Ubunge wa Jimbo la Arusha Mjini kupitia Chama cha Mapinduzi (CCM), Paul Makonda, amesema atahakikisha vijana wanapatiwa fursa mbalimbali za kiuchumi ili waweze kujiajiri na kushiriki kikamilifu katika maendeleo ya Taifa.

Akizungumza wakati alipokuwa akipita mtaa kwa mtaa kuhamasisha wananchi kupiga kura siku ya Tarehe 29 Oktoba, Makonda alisema serikali itawajengea uwezo vijana kufanya shughuli zao kwa ufanisi na kupunguza changamoto za ajira.

“Tutahakikisha tunamuwezesha kijana afanye majukumu yake vizuri. Vijana wapo wanaofanya kazi kwa ajili ya hali ngumu ya maisha, tutahakikisha tunaibua fursa za kiuchumi ili kila kijana awe na shughuli za kufanya,” alisema Makonda.

Aidha, alisisitiza kuwa usalama wa nchi ni jukumu la wananchi wote, akihimiza jamii kushirikiana katika kuwalinda watoto na kuhakikisha maeneo wanayoishi yanakuwa salama.

“Watoto wanaofanya matukio ni watoto wetu, kila mmoja anatakiwa kuwa sehemu ya ulinzi wa watoto kuanzia ngazi za familia,” aliongeza.

Makonda pia alisema watahakikisha thamani ya mabalozi na ngazi za mashina inarejeshwa, ili wawe walinzi wa ulinzi na usalama katika maeneo yao chini ya usimamizi wa wenyeviti wa mitaa na vijiji kuhakikisha kila kaya inakuwa salama.

Akizungumzia mikopo, alisema ndani ya halmashauri kuna aina nne za mikopo inayotokana na makusanyo ya mapato ya ndani ambayo ni kwa wanawake, vijana, vikundi maalum (special groups) na kupitia ofisi mbalimbali za serikali kama Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Ofisi ya Waziri Mkuu na mikopo ya uwezeshaji kiuchumi. Aliahidi kuhakikisha wananchi wanaelewa taratibu za mikopo hiyo na kuipata kwa urahisi.

Kuhusu kupanda kwa bei ya gesi za kupikia, Makonda alisema Tanzania bado haijafikia kiwango cha uzalishaji wa kutosha kwani gesi nyingi zinaagizwa kutoka nje ya nchi, huku matumizi yake yakiongezeka zaidi ya uzalishaji wa ndani.

Vilevile, Makonda alisema jiji la Arusha bado lipo nyuma katika miundombinu ya barabara, hivyo atahakikisha miundombinu hiyo inaboreshwa ili kurahisisha shughuli za kiuchumi na kijamii kwa wananchi.

Akihitimisha, Makonda aliwakumbusha wananchi kuwa tarehe 29 Oktoba ni siku muhimu ya kupiga kura, akiwataka wajitokeze kwa wingi kushiriki katika zoezi hilo.

“Tarehe 29 ndiyo siku ya kupiga kura. Twende tukaombe kura kwa Dkt. Samia, wabunge na madiwani wetu. Vituo vimesogezwa karibu na makazi yetu jumla ya vituo 1,051 katika Jimbo la Arusha,” alisema Makonda.

Aliongeza kuwa kampeni yao ni ya mlango kwa mlango, wakihamasisha wananchi wote kujitokeza.

“Wanaokuja hapa ni wakazi wa jiji la Arusha, na wengine siyo wakazi wa jiji hili. Usisahau kuwaombea kura pia madiwani wa huko na Dkt. Samia. Ukikutana na bodaboda, mtu wa hoteli, au mfanyabiashara msemeshe, tuwahimize wote kujitokeza kupiga kura Oktoba 29,” alisisitiza.

Makonda pia aliwahimiza wale waliopoteza vitambulisho vya kupigia kura wasikate tamaa.

“Kuna wengine wamepoteza vitambulisho vyao. Chukua kile chenye majina yanayofanana na yale uliyotumia kujiandikisha. Ukifika kituoni utamuona msaidizi atakayekusaidia. Muhimu ni kushiriki kwenye kura hii ya kihistoria,” alihitimisha.

Continue Reading
Click to comment
0 0 votes
Article Rating
Subscribe
Notify of
guest
0 Comments
Oldest
Newest Most Voted
Inline Feedbacks
View all comments

News

Wanawake 142 waanza mafunzo ya Female Future Programme Dar es Salaam

Published

on

By

Na Mwandishi wetu, News info

Zaidi ya wanawake 142 wamepokelewa rasmi kushiriki toleo la 12 la programu ya mafunzo ya uongozi kwa wanawake, Female Future Programme (FFP), iliyofanyika jijini Dar es Salaam.

Mafunzo hayo ya kiutendaji yameandaliwa na Chama cha Waajiri Tanzania (ATE) kwa kushirikiana na Taasisi ya Usimamizi ya Afrika Mashariki na Kusini (ESAMI).

Mkurugenzi Mtendaji wa ATE, Bi. Suzanne Ndomba-Doran amesema programu hiyo imekuwa na mchango mkubwa kwa zaidi ya wanawake 800 waliokwisha pata mafunzo kwa zaidi ya muongo mmoja, na sasa inaendeshwa katika nchi sita kwa ufadhili wa NHO, huku akiwahamasisha washiriki kushiriki kikamilifu safari ya miezi tisa ya mafunzo. Aidha, Naibu Mkurugenzi Mkuu wa ESAMI, Dkt. David Kalaba amesema jamii inahitaji wanawake viongozi wenye kujiamini na uwezo mkubwa katika kipindi hiki cha mabadiliko ya haraka, akisisitiza umuhimu wa mtazamo wa kimataifa, kujifunza na kuendana na mabadiliko pamoja na uwezo wa kusimamia utofauti, kutatua migogoro na kutoa thamani kwa wateja.

Kwa upande wake, Meneja wa Upstream wa IFC, Bw. Sam Nganga aliyemwakilisha Meneja wa Nchi, Bi. Martine Valcin amesema taasisi hiyo inaendelea kuhakikisha wanawake wanapewa nafasi katika ngazi za juu za uongozi ili kukuza ushirikishwaji, huku akiwahimiza washiriki kujisimamia na kutumia kikamilifu mafunzo hayo.

Katika hafla hiyo pia kulikuwa na mjadala wa jopo kuhusu wanawake katika uongozi uliowashirikisha wataalamu mbalimbali wa rasilimali watu na uongozi kutoka taasisi tofauti, ambapo ilisisitizwa kuwa kuchanganya uzoefu wa vizazi tofauti vya wanawake kazini huleta matokeo chanya pamoja na umuhimu wa kujifunza ujuzi mpya na kuimarisha mentorship baada ya mafunzo.

Washiriki wa kundi la 12 walihimizwa kujenga mitandao imara ya kitaaluma, huku taasisi na makampuni yakitakiwa kutambua upekee wa kila mwanamke badala ya kuwaona kama kundi moja.

Akihitimisha, Mjumbe wa Bodi ya ATE, Bw. Gasper Kikui amesema sekta isiyo rasmi bado ina changamoto nyingi za uongozi na kuwataka washiriki kuyachukulia mafunzo hayo kwa uzito ili kuleta mabadiliko chanya.

Continue Reading

News

Dkt Samia: Vijana wanufaike na uwekezaji katika mawasiliano

Published

on

By

Na Mwandishi wetu, News info

Rais Dkt Samia Suluhu Hassan, ametaka vijana wanufaike ipasavyo na huduma za mkongo wa Taifa wa mawasiliano, hasa katika maeneo ya kukuza ubunifu, ujuzi wa kidigitali na fursa za ajira.

Ametaka Wizara ya Mawasiliano na Teknolojia ya Habari na Wizara ya Nchi, Ofisi ya Rais, Maendeleo ya Vijana, zishirikiane na wadau wa sekta ya teknolojia ili vijana wapate manufaa hayo.

Dkt Samia ameyasema hayo leo, Ijumaa Aprili 10, 2026 jijini Dodoma, wakati wa uzinduzi huo, ukiambatana na kuunganisha huduma za mkongo wa Taifa wa mawasiliano katika Wilaya 85.

“Uwekezaji huu kwa vijana ni muhimu kwa sababu dunia ya teknolojia ni ya kwao. Dunia hii ipo viganjani mwao na ndiyo mfumo wa maisha yao. Ni lazima tuwawezeshe na kuwahamasisha kutumia mifumo hii ili waweze kukua kiuchumi na kijamii,” amesema.

Continue Reading

News

Dkt Samia azindua minara 758, kuwanufaisha zaidi ya wananchi milioni nane

Published

on

By

Na Mwandishi wetu, News info

Zaidi ya wananchi milioni 8.5 hususan wanaoishi mipakani na vijijini, wanatarajiwa kuondolewa changamoto ya mtandao, baada ya Rais Dkt Samia Suluhu Hassan, kuzindua minara 758 ya mawasiliano iliyojengwa katika maeneo mbalimbali nchini.

Uzinduzi huo umefanyika leo Ijumaa Aprili 10, 2026 jijini Dodoma, ukiambatana na kuunganisha huduma za mkongo wa Taifa wa mawasiliano katika Wilaya 85, ikiwa ni juhudi za Serikali kuimarisha uchumi wa kidijitali na kuongeza huduma za mawasiliano.

Akizungumza wakati wa uzinduzi huo, Dkt Samia amesema uwekezaji huo umetokana na ushirikiano kati ya Serikali na wadau wa sekta ya mawasiliano ili kuhakikisha huduma za mawasiliano zinawafikia wananchi kwa ubora unaokidhi mahitaji ya teknolojia ya kisasa na kwa gharama nafuu.

Amesema kukamilika kwa ujenzi wa minara hiyo kutachochea ushiriki wa wananchi katika uchumi wa kidijitali na kufungua fursa mpya za ajira, kuboresha utoaji wa huduma za kijamii na kuharakisha maendeleo ya Taifa.

“Mawasiliano si tena huduma ya anasa kama ilivyokuwa zamani. Leo hii ni uti wa mgongo wa uchumi wa kisasa na daraja la fursa kwa wananchi katika nyanja mbalimbali za maendeleo,” amesema

Continue Reading

Trending

Copyright © 2025 Newsinfo.