Connect with us

News

Viongozi wa dini waendelea kuhimiza amani uchaguzi mkuu

Published

on

Na Mwandishi wetu, Dar es salaam

VIONGOZI wa dini nchini wameendelea kuhimiza umuhimu wa kudumisha amani, umoja na uzalendo kuelekea Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 29, 2025, wakisisitiza kuwa amani ndiyo msingi wa ustawi wa taifa na ibada halisi kwa Mungu.

Wakizungumza leo Jumatatu, Oktoba 27, 2025, katika Kongamano la Amani la Kitaifa kuelekea Uchaguzi Mkuu, lililofanyika katika Ukumbi wa Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNICC), jijini Dar es Salaam, viongozi hao wamesema jukumu la kulinda amani ni la kila Mtanzania, bila kujali dini wala itikadi.

Sheikh Mkuu wa Tanzania, Dkt. Abubakar Zuberi, amesema viongozi wa dini wana wajibu wa kuhakikisha jamii inaendelea kuwa na amani, upendo na uzalendo, hasa katika kipindi nyeti cha uchaguzi.

“Sisi kama viongozi wa dini tunalazimika kufanya kazi waliyofanya mitume kuhakikisha amani inakuwepo ulimwenguni. Ukiwa na uzalendo utatunza amani, na kutunza amani ndiyo dini,” amesema Sheikh Mkuu.

Ameeleza kuwa makongamano ya amani yaliyofanyika katika kanda mbalimbali za nchi yamekuwa jukwaa muhimu la kuwakumbusha Watanzania juu ya wajibu wa kulinda amani na kuendeleza mshikamano wa kitaifa.

Kwa upande wake, Naibu Katibu Mkuu wa Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania (TEC), Padri Chesco Msaga, amesema amani ya kweli huanzia ndani ya moyo wa mtu binafsi kabla ya kuonekana katika jamii.

“Amani ya kweli inaanzia ndani ya roho. Kama sina amani moyoni siwezi nikapeleka amani kwa mtu mwingine,” amesema.

Mkurugenzi wa Al Hikma Foundation, Sheikh Nurdin Kishki, amewataka Watanzania kuendelea kulitetea taifa kwa maneno na matendo ya kizalendo, akisema ni kosa kwa mtu kutaka kuvuruga amani kwa kisingizio cha maoni binafsi.

“Siku hizi ukisimama kulitetea taifa lako unaambiwa umepewa bahasha. Lakini nataka kuuliza, wale wanaotaka kuvunja amani wanapewa na nani?” amehoji.

Naye Mwenyekiti wa Jumuiya ya Makanisa ya Tanzania (JMAT-TAIFA), Alhad Mussa Salum, ametoa wito kwa wazazi na viongozi kuendelea kuwaelimisha vijana, hasa wa kizazi cha Gen Z, juu ya thamani ya nchi na madhara ya vurugu.

“Changamoto hazitatuliki kwa uharibifu bali kwa utaratibu. Tuwasihi vijana wetu kwamba kuiharibu nchi kisha kufikiria kuitengeneza upya si jambo la busara,” amesema.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Makanisa ya Kipentekosti Tanzania (CPCT), Dk. Vernon Fernandes, amesema rasilimali na mafanikio yaliyopo nchini hayawezi kudumu bila uwepo wa amani, akiwataka wananchi kujitokeza kupiga kura kwa utulivu.

Wakati huo huo, Serikali imetoa shukrani kwa viongozi wa dini kupitia Kamati ya Amani kwa juhudi zao za kudumisha utulivu na mshikamano wa kitaifa.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Mipango na Uwekezaji), Prof. Kitila Mkumbo, aliyemwakilisha Makamu wa Rais, Dk. Philip Mpango, wakati wa kufunga kongamano hilo, amesema makongamano ya amani yamekuwa chachu ya kuimarisha imani ya wananchi kuelekea uchaguzi.

“Tafiti zinaonyesha wananchi wengi wanawaamini zaidi viongozi wa dini wanapokuwa na changamoto zao. Kwa hiyo mchango wenu ni mkubwa sana katika kuhakikisha Watanzania wanashiriki uchaguzi kwa amani,” amesema Prof. Mkumbo.

Ameongeza kuwa huu ni uchaguzi wa 14 tangu Tanzania ianze mfumo wa vyama vingi, hivyo ni kipindi muhimu cha kuendelea kudumisha amani kama urithi wa taifa.

Kongamano hilo limehitimisha mfululizo wa makongamano ya amani yaliyofanyika nchini kupitia kanda zote Kusini, Kaskazini, Kati, Magharibi na Nyanda za Juu Kusini yakiratibiwa na Kamati ya Amani ya Kitaifa.

Continue Reading
Click to comment
0 0 votes
Article Rating
Subscribe
Notify of
guest
0 Comments
Oldest
Newest Most Voted
Inline Feedbacks
View all comments

News

Wanawake 142 waanza mafunzo ya Female Future Programme Dar es Salaam

Published

on

By

Na Mwandishi wetu, News info

Zaidi ya wanawake 142 wamepokelewa rasmi kushiriki toleo la 12 la programu ya mafunzo ya uongozi kwa wanawake, Female Future Programme (FFP), iliyofanyika jijini Dar es Salaam.

Mafunzo hayo ya kiutendaji yameandaliwa na Chama cha Waajiri Tanzania (ATE) kwa kushirikiana na Taasisi ya Usimamizi ya Afrika Mashariki na Kusini (ESAMI).

Mkurugenzi Mtendaji wa ATE, Bi. Suzanne Ndomba-Doran amesema programu hiyo imekuwa na mchango mkubwa kwa zaidi ya wanawake 800 waliokwisha pata mafunzo kwa zaidi ya muongo mmoja, na sasa inaendeshwa katika nchi sita kwa ufadhili wa NHO, huku akiwahamasisha washiriki kushiriki kikamilifu safari ya miezi tisa ya mafunzo. Aidha, Naibu Mkurugenzi Mkuu wa ESAMI, Dkt. David Kalaba amesema jamii inahitaji wanawake viongozi wenye kujiamini na uwezo mkubwa katika kipindi hiki cha mabadiliko ya haraka, akisisitiza umuhimu wa mtazamo wa kimataifa, kujifunza na kuendana na mabadiliko pamoja na uwezo wa kusimamia utofauti, kutatua migogoro na kutoa thamani kwa wateja.

Kwa upande wake, Meneja wa Upstream wa IFC, Bw. Sam Nganga aliyemwakilisha Meneja wa Nchi, Bi. Martine Valcin amesema taasisi hiyo inaendelea kuhakikisha wanawake wanapewa nafasi katika ngazi za juu za uongozi ili kukuza ushirikishwaji, huku akiwahimiza washiriki kujisimamia na kutumia kikamilifu mafunzo hayo.

Katika hafla hiyo pia kulikuwa na mjadala wa jopo kuhusu wanawake katika uongozi uliowashirikisha wataalamu mbalimbali wa rasilimali watu na uongozi kutoka taasisi tofauti, ambapo ilisisitizwa kuwa kuchanganya uzoefu wa vizazi tofauti vya wanawake kazini huleta matokeo chanya pamoja na umuhimu wa kujifunza ujuzi mpya na kuimarisha mentorship baada ya mafunzo.

Washiriki wa kundi la 12 walihimizwa kujenga mitandao imara ya kitaaluma, huku taasisi na makampuni yakitakiwa kutambua upekee wa kila mwanamke badala ya kuwaona kama kundi moja.

Akihitimisha, Mjumbe wa Bodi ya ATE, Bw. Gasper Kikui amesema sekta isiyo rasmi bado ina changamoto nyingi za uongozi na kuwataka washiriki kuyachukulia mafunzo hayo kwa uzito ili kuleta mabadiliko chanya.

Continue Reading

News

Dkt Samia: Vijana wanufaike na uwekezaji katika mawasiliano

Published

on

By

Na Mwandishi wetu, News info

Rais Dkt Samia Suluhu Hassan, ametaka vijana wanufaike ipasavyo na huduma za mkongo wa Taifa wa mawasiliano, hasa katika maeneo ya kukuza ubunifu, ujuzi wa kidigitali na fursa za ajira.

Ametaka Wizara ya Mawasiliano na Teknolojia ya Habari na Wizara ya Nchi, Ofisi ya Rais, Maendeleo ya Vijana, zishirikiane na wadau wa sekta ya teknolojia ili vijana wapate manufaa hayo.

Dkt Samia ameyasema hayo leo, Ijumaa Aprili 10, 2026 jijini Dodoma, wakati wa uzinduzi huo, ukiambatana na kuunganisha huduma za mkongo wa Taifa wa mawasiliano katika Wilaya 85.

“Uwekezaji huu kwa vijana ni muhimu kwa sababu dunia ya teknolojia ni ya kwao. Dunia hii ipo viganjani mwao na ndiyo mfumo wa maisha yao. Ni lazima tuwawezeshe na kuwahamasisha kutumia mifumo hii ili waweze kukua kiuchumi na kijamii,” amesema.

Continue Reading

News

Dkt Samia azindua minara 758, kuwanufaisha zaidi ya wananchi milioni nane

Published

on

By

Na Mwandishi wetu, News info

Zaidi ya wananchi milioni 8.5 hususan wanaoishi mipakani na vijijini, wanatarajiwa kuondolewa changamoto ya mtandao, baada ya Rais Dkt Samia Suluhu Hassan, kuzindua minara 758 ya mawasiliano iliyojengwa katika maeneo mbalimbali nchini.

Uzinduzi huo umefanyika leo Ijumaa Aprili 10, 2026 jijini Dodoma, ukiambatana na kuunganisha huduma za mkongo wa Taifa wa mawasiliano katika Wilaya 85, ikiwa ni juhudi za Serikali kuimarisha uchumi wa kidijitali na kuongeza huduma za mawasiliano.

Akizungumza wakati wa uzinduzi huo, Dkt Samia amesema uwekezaji huo umetokana na ushirikiano kati ya Serikali na wadau wa sekta ya mawasiliano ili kuhakikisha huduma za mawasiliano zinawafikia wananchi kwa ubora unaokidhi mahitaji ya teknolojia ya kisasa na kwa gharama nafuu.

Amesema kukamilika kwa ujenzi wa minara hiyo kutachochea ushiriki wa wananchi katika uchumi wa kidijitali na kufungua fursa mpya za ajira, kuboresha utoaji wa huduma za kijamii na kuharakisha maendeleo ya Taifa.

“Mawasiliano si tena huduma ya anasa kama ilivyokuwa zamani. Leo hii ni uti wa mgongo wa uchumi wa kisasa na daraja la fursa kwa wananchi katika nyanja mbalimbali za maendeleo,” amesema

Continue Reading

Trending

Copyright © 2025 Newsinfo.