Connect with us

News

Mashirika ya umma yasiyofanya vizuri kufutwa au kuunganishwa

Published

on

Na Mwandishi wetu, News Info Online

Dar es Salaam. Serikali imetoa onyo kwa taasisi na mashirika ya umma yasiyoonesha ufanisi, ikisema yako hatarini kufutwa au kuunganishwa endapo hayatachukua hatua madhubuti za kuboresha utendaji wao.

Onyo hilo lilitolewa Ijumaa, Disemba 5, 2025, na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais—Mipango na Uwekezaji, Prof. Kitila Mkumbo, wakati wa ziara yake katika Ofisi ya Msajili wa Hazina (OMH) jijini Dar es Salaam.

Akizungumza na waandishi wa habari mara baada ya kufanya kikao cha ndani na menejimenti ya OMH ikiongozwa na Msajili wa Hazina, Bw. Nehemiah Mchechu, Prof. Mkumbo alisema haiingii akilini kuona baadhi ya mashirika ya umma yakishindwa kutoa gawio stahiki licha ya uwekezaji mkubwa uliofanywa na Serikali.

Alisema Serikali itatoa muda maalum kwa taasisi husika kujirekebisha kabla ya kuchukua maamuzi ya kuyaunganisha au kuyafuta pale itakapobidi.

“Ni afadhali kuwa na mashirika machache ya biashara, lakini yanayotoa gawio stahiki kwa Serikali,” alisisitiza Prof. Mkumbo, ambaye aliambatana na Naibu Waziri wa Mipango na Uwekezaji, Dk. Pius Stephen Chaya, na Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, Dk. Tausi Kida.

Kwa mujibu wa OMH, Serikali inamiliki hisa katika taasisi na kampuni 308, ambapo 91 pekee ndizo zinazofanya biashara na 217 hazifanyi.
Prof. Kitila alisema Serikali inataka kuona wananchi wakifaidi matunda ya uwekezaji wake wa Sh92.3 trilioni uliofanywa katika mashirika ya umma.

Katika mwaka wa fedha 2024/25, OMH ilikusanya Sh1.028 trilioni kama gawio kutoka kwa taasisi za umma na kampuni ambazo Serikali ina umiliki wa hisa chache — kiasi kilicho rekodi historia mpya tangu kuanzishwa kwa ofisi hiyo mwaka 1959.

Hata hivyo, Serikali inaamini bado kuna nafasi kubwa ya kukusanya zaidi.

Kwa muktadha huo, Serikali imeiwekea OMH lengo la kukusanya Sh1.7 trilioni katika mwaka wa fedha 2025/26, huku ofisi hiyo yenyewe ikijiwekea lengo la ndani la kukusanya hadi Sh2 trilioni kutokana na mageuzi inayoyasimamia kwenye mashirika ya umma.

Prof. Mkumbo alisema kwamba Serikali itaongeza ufanisi zaidi kwa kuhakikisha upatikanaji wa watendaji na wajumbe wa bodi za mashirika ya umma unafanyika kwa uwazi na ushindani.

“Kazi yangu ni kuhakikisha tunakuwa na Sheria bora ya Uwekezaji wa Umma itakayo chochea ufanisi wa mashirika ya umma,” alisema.

Alisema anaamini maboresho ya muswada huo yatafanyika kwa haraka na hatimaye kusomwa kwa mara ya pili bungeni katika siku za karibuni.

Aidha, alibainisha kuwa lengo la Serikali ni kubadili sura, ufanisi na utendaji wa mashirika ya umma ili yaweze kutoa huduma bora na kuchochea uwekezaji.

Kwa upande wake, Msajili wa Hazina, Bw. Nehemiah Mchechu, alisema OMH imejipanga kuendelea kuimarisha mashirika ya umma ili kuongeza ufanisi katika huduma na uwekezaji.

“Usimamizi bora wa utendaji wa Taasisi na Mashirika ya Umma ni chachu ya mageuzi katika uendeshaji wa sekta hii,” alisema Bw. Mchechu.

Aliongeza kuwa uimarishaji wa usimamizi huo utaongeza uzalishaji, kuboresha uchumi na kuongeza mapato ya kodi na yasiyo ya kodi — ambayo ni muhimu katika kuwezesha Serikali kutekeleza majukumu yake.

Continue Reading
Click to comment
0 0 votes
Article Rating
Subscribe
Notify of
guest
0 Comments
Oldest
Newest Most Voted
Inline Feedbacks
View all comments

News

Wanawake 142 waanza mafunzo ya Female Future Programme Dar es Salaam

Published

on

By

Na Mwandishi wetu, News info

Zaidi ya wanawake 142 wamepokelewa rasmi kushiriki toleo la 12 la programu ya mafunzo ya uongozi kwa wanawake, Female Future Programme (FFP), iliyofanyika jijini Dar es Salaam.

Mafunzo hayo ya kiutendaji yameandaliwa na Chama cha Waajiri Tanzania (ATE) kwa kushirikiana na Taasisi ya Usimamizi ya Afrika Mashariki na Kusini (ESAMI).

Mkurugenzi Mtendaji wa ATE, Bi. Suzanne Ndomba-Doran amesema programu hiyo imekuwa na mchango mkubwa kwa zaidi ya wanawake 800 waliokwisha pata mafunzo kwa zaidi ya muongo mmoja, na sasa inaendeshwa katika nchi sita kwa ufadhili wa NHO, huku akiwahamasisha washiriki kushiriki kikamilifu safari ya miezi tisa ya mafunzo. Aidha, Naibu Mkurugenzi Mkuu wa ESAMI, Dkt. David Kalaba amesema jamii inahitaji wanawake viongozi wenye kujiamini na uwezo mkubwa katika kipindi hiki cha mabadiliko ya haraka, akisisitiza umuhimu wa mtazamo wa kimataifa, kujifunza na kuendana na mabadiliko pamoja na uwezo wa kusimamia utofauti, kutatua migogoro na kutoa thamani kwa wateja.

Kwa upande wake, Meneja wa Upstream wa IFC, Bw. Sam Nganga aliyemwakilisha Meneja wa Nchi, Bi. Martine Valcin amesema taasisi hiyo inaendelea kuhakikisha wanawake wanapewa nafasi katika ngazi za juu za uongozi ili kukuza ushirikishwaji, huku akiwahimiza washiriki kujisimamia na kutumia kikamilifu mafunzo hayo.

Katika hafla hiyo pia kulikuwa na mjadala wa jopo kuhusu wanawake katika uongozi uliowashirikisha wataalamu mbalimbali wa rasilimali watu na uongozi kutoka taasisi tofauti, ambapo ilisisitizwa kuwa kuchanganya uzoefu wa vizazi tofauti vya wanawake kazini huleta matokeo chanya pamoja na umuhimu wa kujifunza ujuzi mpya na kuimarisha mentorship baada ya mafunzo.

Washiriki wa kundi la 12 walihimizwa kujenga mitandao imara ya kitaaluma, huku taasisi na makampuni yakitakiwa kutambua upekee wa kila mwanamke badala ya kuwaona kama kundi moja.

Akihitimisha, Mjumbe wa Bodi ya ATE, Bw. Gasper Kikui amesema sekta isiyo rasmi bado ina changamoto nyingi za uongozi na kuwataka washiriki kuyachukulia mafunzo hayo kwa uzito ili kuleta mabadiliko chanya.

Continue Reading

News

Dkt Samia: Vijana wanufaike na uwekezaji katika mawasiliano

Published

on

By

Na Mwandishi wetu, News info

Rais Dkt Samia Suluhu Hassan, ametaka vijana wanufaike ipasavyo na huduma za mkongo wa Taifa wa mawasiliano, hasa katika maeneo ya kukuza ubunifu, ujuzi wa kidigitali na fursa za ajira.

Ametaka Wizara ya Mawasiliano na Teknolojia ya Habari na Wizara ya Nchi, Ofisi ya Rais, Maendeleo ya Vijana, zishirikiane na wadau wa sekta ya teknolojia ili vijana wapate manufaa hayo.

Dkt Samia ameyasema hayo leo, Ijumaa Aprili 10, 2026 jijini Dodoma, wakati wa uzinduzi huo, ukiambatana na kuunganisha huduma za mkongo wa Taifa wa mawasiliano katika Wilaya 85.

“Uwekezaji huu kwa vijana ni muhimu kwa sababu dunia ya teknolojia ni ya kwao. Dunia hii ipo viganjani mwao na ndiyo mfumo wa maisha yao. Ni lazima tuwawezeshe na kuwahamasisha kutumia mifumo hii ili waweze kukua kiuchumi na kijamii,” amesema.

Continue Reading

News

Dkt Samia azindua minara 758, kuwanufaisha zaidi ya wananchi milioni nane

Published

on

By

Na Mwandishi wetu, News info

Zaidi ya wananchi milioni 8.5 hususan wanaoishi mipakani na vijijini, wanatarajiwa kuondolewa changamoto ya mtandao, baada ya Rais Dkt Samia Suluhu Hassan, kuzindua minara 758 ya mawasiliano iliyojengwa katika maeneo mbalimbali nchini.

Uzinduzi huo umefanyika leo Ijumaa Aprili 10, 2026 jijini Dodoma, ukiambatana na kuunganisha huduma za mkongo wa Taifa wa mawasiliano katika Wilaya 85, ikiwa ni juhudi za Serikali kuimarisha uchumi wa kidijitali na kuongeza huduma za mawasiliano.

Akizungumza wakati wa uzinduzi huo, Dkt Samia amesema uwekezaji huo umetokana na ushirikiano kati ya Serikali na wadau wa sekta ya mawasiliano ili kuhakikisha huduma za mawasiliano zinawafikia wananchi kwa ubora unaokidhi mahitaji ya teknolojia ya kisasa na kwa gharama nafuu.

Amesema kukamilika kwa ujenzi wa minara hiyo kutachochea ushiriki wa wananchi katika uchumi wa kidijitali na kufungua fursa mpya za ajira, kuboresha utoaji wa huduma za kijamii na kuharakisha maendeleo ya Taifa.

“Mawasiliano si tena huduma ya anasa kama ilivyokuwa zamani. Leo hii ni uti wa mgongo wa uchumi wa kisasa na daraja la fursa kwa wananchi katika nyanja mbalimbali za maendeleo,” amesema

Continue Reading

Trending

Copyright © 2025 Newsinfo.