Connect with us

News

NMB Yazindua Jukwaa la JASIRI Kukuza Uwezo wa Wanawake Kiuchumi

Published

on

Na Mwandishi wetu, News Info Online

Benki ya NMB imezindua jukwaa la JASIRI lenye lengo la kuwawezesha wanawake kiuchumi kwa kuwapatia fursa za elimu ya fedha, huduma za kifedha, ushirikiano wa kibiashara pamoja na majukwaa ya kujifunza na kushirikiana katika kukuza biashara zao.

Uzinduzi huo umefanyika sambamba na maadhimisho ya Mwezi wa Wanawake Duniani ikiwa ni sehemu ya jitihada za benki hiyo kukuza uchumi jumuishi nchini.

Akizungumza wakati wa uzinduzi huo, Afisa Mkuu wa Wateja Binafsi na Biashara wa NMB, Bw. Filbert Mponzi, amesema jukwaa la JASIRI linaonesha dhamira ya benki hiyo katika kuwawezesha wanawake ambao wameendelea kuwa nguzo muhimu katika kukuza uchumi wa Tanzania.

“Takwimu zinaonesha kuwa wanawake wanamiliki au kuendesha karibu nusu ya biashara nchini, lakini bado wengi wao wanakabiliwa na changamoto ya upatikanaji wa mitaji, mitandao ya biashara pamoja na fursa za kukuza biashara zao.”

Amesema kuwa NMB inaamini uwezeshaji wa wanawake hauishii katika utoaji wa huduma za kifedha pekee, bali pia ni kujenga mazingira yatakayowawezesha wanawake kuunganishwa, kujifunza na kushirikiana ili kufungua fursa zaidi za kukuza biashara na kutimiza ndoto zao.

Mponzi ameeleza kuwa kupitia jukwaa la JASIRI, wanawake watapata nafasi ya kushiriki katika mazungumzo ya ushirikiano yatakayosaidia kubuni fursa mbalimbali zinazohusisha elimu ya fedha, huduma za kifedha, ujasiriamali pamoja na ushirikiano wa kimkakati.

Ameongeza kuwa mpango huo umeimarishwa kupitia tafiti na tathmini zilizofanywa kwa kushirikiana na washirika wa NMB, IFC na Mastercard, ili kubuni suluhisho zinazokidhi mahitaji ya wanawake katika kukuza biashara zao.

“Kuwekeza katika suluhisho zinazowawezesha wanawake ni fursa muhimu kijamii na kiuchumi, kwani wanawake ni miongoni mwa makundi yanayokua kwa kasi katika ujasiriamali na pia ni wahusika wakuu katika maamuzi mengi ya kifedha ndani ya familia nyingi nchini.”

Hata hivyo, amesema bado kuna changamoto katika upatikanaji wa mitaji, masoko na maarifa ya kifedha, huku akibainisha kuwa kwa mujibu wa Benki ya Maendeleo ya Afrika, kuna pengo la ufadhili linalokadiriwa kufikia dola za Marekani bilioni 42 kila mwaka katika Afrika Kusini mwa Jangwa la Sahara.

“NMB inaona fursa katika kusaidia kuziba pengo hilo kwa kubuni bidhaa, huduma na majukwaa yanayolenga mahitaji ya wanawake” amesema Mponzi na kuongeza kuwa;

“Wanawake wanapopata ujumuishaji wa kifedha wana uwezo mkubwa wa kukuza biashara zao, kuweka akiba zaidi, kuwekeza katika familia zao na kuchangia kujenga jamii imara na yenye ustahimilivu.”

Aidha, ametoa pongezi kwa wanawake wote wa Tanzania kwa mchango wao mkubwa katika familia, jamii na uchumi wa taifa, akisema benki hiyo itaendelea kuwaunga mkono kupitia huduma bora za kifedha, elimu pamoja na fursa mbalimbali zitakazowawezesha kukua na kufanikiwa.

Kwa upande wake, Meneja Mwandamizi wa Masoko ya Wateja Binafsi na Biashara wa NMB, Irene Mutigazi, amesema jukwaa la JASIRI ni wito kwa wanawake kuamini katika uwezo wao na kuthubutu kufuatilia ndoto zao.

Amesema kupitia jukwaa hilo pamoja na Kochi la Orange la JASIRI, wanawake wataalikwa kushiriki mazungumzo, kupata ushauri, elimu ya fedha na fursa mbalimbali za kukuza biashara zao ikiwa ni sehemu ya kampeni ya benki hiyo ya “Tuyajenge.”

Naye Meneja Mwandamizi wa Bidhaa za Amana wa NMB, Beatrice Mwambije, amesema kupitia jukwaa la JASIRI benki hiyo imeandaa suluhisho mbalimbali za kifedha zinazolenga kuwawezesha wanawake, ikiwemo mikopo ya biashara, mikopo ya kidigitali, mikopo ya vikundi pamoja na bidhaa za akiba.

Ameongeza kuwa sambamba na huduma hizo, wanawake watapatiwa mafunzo ya elimu ya fedha, ushauri wa biashara pamoja na fursa za kujenga mitandao ya kibiashara ili kuwasaidia kukuza biashara zao na kufikia uhuru wa kifedha.

Afisa Mtendaji Mkuu wa Benki ya NMB, Ruth Zaipuna (wa tatu kushoto) akiwa pamoja na wadau wa Jukwaa Maalum la Uwezeshaji Wanawake Kiuchumi liitwalo NMB Mwanamke Jasiri baada ya uzinduzi uliofanyika jijini Dar es Salaam Machi 12 2026. Wengine ni Mwakilishi wa Shirika la Kimataifa la Fedha (IFC), Louise Gardiner (wa pili kushoto), Mwakilishi Mkazi wa MasterCard Tanzania Moses Alphonse ( kulia), Afisa Mkuu wa Wateja Binafsi na Biashara wa NMB, Filbert Mponzi (kushoto), Mtangazaji wa radio, Najma Paul (wa tatu kulia) na Mwakilishi wa IFC, Joy Kemibaro (wa pili kulia).

Continue Reading
Click to comment
0 0 votes
Article Rating
Subscribe
Notify of
guest
0 Comments
Oldest
Newest Most Voted
Inline Feedbacks
View all comments

News

Wanawake 142 waanza mafunzo ya Female Future Programme Dar es Salaam

Published

on

By

Na Mwandishi wetu, News info

Zaidi ya wanawake 142 wamepokelewa rasmi kushiriki toleo la 12 la programu ya mafunzo ya uongozi kwa wanawake, Female Future Programme (FFP), iliyofanyika jijini Dar es Salaam.

Mafunzo hayo ya kiutendaji yameandaliwa na Chama cha Waajiri Tanzania (ATE) kwa kushirikiana na Taasisi ya Usimamizi ya Afrika Mashariki na Kusini (ESAMI).

Mkurugenzi Mtendaji wa ATE, Bi. Suzanne Ndomba-Doran amesema programu hiyo imekuwa na mchango mkubwa kwa zaidi ya wanawake 800 waliokwisha pata mafunzo kwa zaidi ya muongo mmoja, na sasa inaendeshwa katika nchi sita kwa ufadhili wa NHO, huku akiwahamasisha washiriki kushiriki kikamilifu safari ya miezi tisa ya mafunzo. Aidha, Naibu Mkurugenzi Mkuu wa ESAMI, Dkt. David Kalaba amesema jamii inahitaji wanawake viongozi wenye kujiamini na uwezo mkubwa katika kipindi hiki cha mabadiliko ya haraka, akisisitiza umuhimu wa mtazamo wa kimataifa, kujifunza na kuendana na mabadiliko pamoja na uwezo wa kusimamia utofauti, kutatua migogoro na kutoa thamani kwa wateja.

Kwa upande wake, Meneja wa Upstream wa IFC, Bw. Sam Nganga aliyemwakilisha Meneja wa Nchi, Bi. Martine Valcin amesema taasisi hiyo inaendelea kuhakikisha wanawake wanapewa nafasi katika ngazi za juu za uongozi ili kukuza ushirikishwaji, huku akiwahimiza washiriki kujisimamia na kutumia kikamilifu mafunzo hayo.

Katika hafla hiyo pia kulikuwa na mjadala wa jopo kuhusu wanawake katika uongozi uliowashirikisha wataalamu mbalimbali wa rasilimali watu na uongozi kutoka taasisi tofauti, ambapo ilisisitizwa kuwa kuchanganya uzoefu wa vizazi tofauti vya wanawake kazini huleta matokeo chanya pamoja na umuhimu wa kujifunza ujuzi mpya na kuimarisha mentorship baada ya mafunzo.

Washiriki wa kundi la 12 walihimizwa kujenga mitandao imara ya kitaaluma, huku taasisi na makampuni yakitakiwa kutambua upekee wa kila mwanamke badala ya kuwaona kama kundi moja.

Akihitimisha, Mjumbe wa Bodi ya ATE, Bw. Gasper Kikui amesema sekta isiyo rasmi bado ina changamoto nyingi za uongozi na kuwataka washiriki kuyachukulia mafunzo hayo kwa uzito ili kuleta mabadiliko chanya.

Continue Reading

News

Dkt Samia: Vijana wanufaike na uwekezaji katika mawasiliano

Published

on

By

Na Mwandishi wetu, News info

Rais Dkt Samia Suluhu Hassan, ametaka vijana wanufaike ipasavyo na huduma za mkongo wa Taifa wa mawasiliano, hasa katika maeneo ya kukuza ubunifu, ujuzi wa kidigitali na fursa za ajira.

Ametaka Wizara ya Mawasiliano na Teknolojia ya Habari na Wizara ya Nchi, Ofisi ya Rais, Maendeleo ya Vijana, zishirikiane na wadau wa sekta ya teknolojia ili vijana wapate manufaa hayo.

Dkt Samia ameyasema hayo leo, Ijumaa Aprili 10, 2026 jijini Dodoma, wakati wa uzinduzi huo, ukiambatana na kuunganisha huduma za mkongo wa Taifa wa mawasiliano katika Wilaya 85.

“Uwekezaji huu kwa vijana ni muhimu kwa sababu dunia ya teknolojia ni ya kwao. Dunia hii ipo viganjani mwao na ndiyo mfumo wa maisha yao. Ni lazima tuwawezeshe na kuwahamasisha kutumia mifumo hii ili waweze kukua kiuchumi na kijamii,” amesema.

Continue Reading

News

Dkt Samia azindua minara 758, kuwanufaisha zaidi ya wananchi milioni nane

Published

on

By

Na Mwandishi wetu, News info

Zaidi ya wananchi milioni 8.5 hususan wanaoishi mipakani na vijijini, wanatarajiwa kuondolewa changamoto ya mtandao, baada ya Rais Dkt Samia Suluhu Hassan, kuzindua minara 758 ya mawasiliano iliyojengwa katika maeneo mbalimbali nchini.

Uzinduzi huo umefanyika leo Ijumaa Aprili 10, 2026 jijini Dodoma, ukiambatana na kuunganisha huduma za mkongo wa Taifa wa mawasiliano katika Wilaya 85, ikiwa ni juhudi za Serikali kuimarisha uchumi wa kidijitali na kuongeza huduma za mawasiliano.

Akizungumza wakati wa uzinduzi huo, Dkt Samia amesema uwekezaji huo umetokana na ushirikiano kati ya Serikali na wadau wa sekta ya mawasiliano ili kuhakikisha huduma za mawasiliano zinawafikia wananchi kwa ubora unaokidhi mahitaji ya teknolojia ya kisasa na kwa gharama nafuu.

Amesema kukamilika kwa ujenzi wa minara hiyo kutachochea ushiriki wa wananchi katika uchumi wa kidijitali na kufungua fursa mpya za ajira, kuboresha utoaji wa huduma za kijamii na kuharakisha maendeleo ya Taifa.

“Mawasiliano si tena huduma ya anasa kama ilivyokuwa zamani. Leo hii ni uti wa mgongo wa uchumi wa kisasa na daraja la fursa kwa wananchi katika nyanja mbalimbali za maendeleo,” amesema

Continue Reading

Trending

Copyright © 2025 Newsinfo.