Connect with us

News

Wakurugenzi Ofisi ya Msajili wa Hazina wapigwa msasa kwa siku tano

Published

on

Na Mwandishi, News Info Online

Ofisi ya Msajili wa Hazina (OTR) kwa kushirikiana na Taasisi ya Wakurugenzi Tanzania (IoDT) imeendesha mafunzo maalum ya uongozi na usimamizi kwa Wakurugenzi na Wakurugenzi Wasaidizi wa Ofisi hiyo, yakilenga kuimarisha uwezo wa menejimenti katika kusimamia rasilimali za umma kwa weledi, uwajibikaji na kwa maslahi mapana ya taifa.

Mafunzo hayo ya siku tano yamefanyika kuanzia Februari 2 hadi 6, 2026 katika Shule ya Uongozi ya Mwl. Julius Nyerere iliyopo Kibaha, yakiwa na dhima kuu ya “Uongozi na Usimamizi Wenye Uwajibikaji kwa Maslahi ya Taifa”.

Kupitia programu hiyo ya siku tano, washiriki walipata fursa ya kujifunza na kujadiliana masuala ya msingi ya uongozi wa kimkakati, utawala bora, uzalendo, maadili ya uongozi wa umma, pamoja na ulinzi wa taasisi dhidi ya hatari za kiutendaji, kimaadili na kiusalama.

Miongoni mwa mada zilizofundishwa ni pamoja na misingi ya utawala bora, uongozi unaozingatia uwajibikaji na matokeo, usimamizi wa uwekezaji wa umma, maamuzi ya kimkakati katika kusimamia taasisi na mashirika ya umma, pamoja na uongozi unaojengwa juu ya maslahi ya taifa na usalama wa nchi.

Aidha, washiriki walijengewa uwezo katika maeneo ya itifaki na adabu kwa viongozi, usimamizi wa hisia (emotional intelligence), majadiliano ya kimkakati, pamoja na uwasilishaji na taswira ya kiongozi katika ngazi ya juu ya Serikali.

Mafunzo hayo pia yaliangazia masuala yanayoathiri uongozi wa kisasa, ikiwemo matumizi ya teknolojia na mifumo ya kidijitali serikalini, uelewa wa bodi mtandao (e-Board), pamoja na misingi ya Akili Unde (Artificial Intelligence) kwa viongozi, hususan fursa, changamoto na masuala ya kimaadili katika maamuzi ya kimkakati.

Vilevile, mada za afya ya viongozi, usimamizi wa msongo wa mawazo na uimara wa kiongozi zilijadiliwa kwa lengo la kuhakikisha ufanisi endelevu wa viongozi katika utekelezaji wa majukumu yao.

Kwa upande wa manufaa, mafunzo haya yanatarajiwa kuongeza mshikamano na ulinganifu wa uongozi ndani ya OMH, kuboresha ubora wa maamuzi ya menejimenti, na kuimarisha uwajibikaji katika usimamizi wa hisa na mali za umma zilizo chini ya Ofisi ya Msajili wa Hazina.

Kupitia uelewa wa pamoja wa dhima ya uongozi na ulezi wa taasisi (institutional stewardship), Wakurugenzi na Wakurugenzi Wasaidizi wamejengewa msingi imara wa kusimamia taasisi na mashirika ya umma kwa ufanisi, nidhamu na kwa kuzingatia vipaumbele vya maendeleo ya Taifa.

Kwa ujumla, ushirikiano kati ya OMH na IoDT katika mafunzo haya ni hatua muhimu katika kujenga uongozi thabiti wa kimkakati ndani ya Serikali, unaoendana na mahitaji ya sasa na ya baadaye ya usimamizi wa rasilimali za umma, na unaochangia moja kwa moja katika kuimarisha utendaji wa OMH kama msimamizi mkuu wa maslahi ya Serikali katika taasisi na mashirika ya umma.

Continue Reading
Click to comment
0 0 votes
Article Rating
Subscribe
Notify of
guest
0 Comments
Oldest
Newest Most Voted
Inline Feedbacks
View all comments

News

Wanawake 142 waanza mafunzo ya Female Future Programme Dar es Salaam

Published

on

By

Na Mwandishi wetu, News info

Zaidi ya wanawake 142 wamepokelewa rasmi kushiriki toleo la 12 la programu ya mafunzo ya uongozi kwa wanawake, Female Future Programme (FFP), iliyofanyika jijini Dar es Salaam.

Mafunzo hayo ya kiutendaji yameandaliwa na Chama cha Waajiri Tanzania (ATE) kwa kushirikiana na Taasisi ya Usimamizi ya Afrika Mashariki na Kusini (ESAMI).

Mkurugenzi Mtendaji wa ATE, Bi. Suzanne Ndomba-Doran amesema programu hiyo imekuwa na mchango mkubwa kwa zaidi ya wanawake 800 waliokwisha pata mafunzo kwa zaidi ya muongo mmoja, na sasa inaendeshwa katika nchi sita kwa ufadhili wa NHO, huku akiwahamasisha washiriki kushiriki kikamilifu safari ya miezi tisa ya mafunzo. Aidha, Naibu Mkurugenzi Mkuu wa ESAMI, Dkt. David Kalaba amesema jamii inahitaji wanawake viongozi wenye kujiamini na uwezo mkubwa katika kipindi hiki cha mabadiliko ya haraka, akisisitiza umuhimu wa mtazamo wa kimataifa, kujifunza na kuendana na mabadiliko pamoja na uwezo wa kusimamia utofauti, kutatua migogoro na kutoa thamani kwa wateja.

Kwa upande wake, Meneja wa Upstream wa IFC, Bw. Sam Nganga aliyemwakilisha Meneja wa Nchi, Bi. Martine Valcin amesema taasisi hiyo inaendelea kuhakikisha wanawake wanapewa nafasi katika ngazi za juu za uongozi ili kukuza ushirikishwaji, huku akiwahimiza washiriki kujisimamia na kutumia kikamilifu mafunzo hayo.

Katika hafla hiyo pia kulikuwa na mjadala wa jopo kuhusu wanawake katika uongozi uliowashirikisha wataalamu mbalimbali wa rasilimali watu na uongozi kutoka taasisi tofauti, ambapo ilisisitizwa kuwa kuchanganya uzoefu wa vizazi tofauti vya wanawake kazini huleta matokeo chanya pamoja na umuhimu wa kujifunza ujuzi mpya na kuimarisha mentorship baada ya mafunzo.

Washiriki wa kundi la 12 walihimizwa kujenga mitandao imara ya kitaaluma, huku taasisi na makampuni yakitakiwa kutambua upekee wa kila mwanamke badala ya kuwaona kama kundi moja.

Akihitimisha, Mjumbe wa Bodi ya ATE, Bw. Gasper Kikui amesema sekta isiyo rasmi bado ina changamoto nyingi za uongozi na kuwataka washiriki kuyachukulia mafunzo hayo kwa uzito ili kuleta mabadiliko chanya.

Continue Reading

News

Dkt Samia: Vijana wanufaike na uwekezaji katika mawasiliano

Published

on

By

Na Mwandishi wetu, News info

Rais Dkt Samia Suluhu Hassan, ametaka vijana wanufaike ipasavyo na huduma za mkongo wa Taifa wa mawasiliano, hasa katika maeneo ya kukuza ubunifu, ujuzi wa kidigitali na fursa za ajira.

Ametaka Wizara ya Mawasiliano na Teknolojia ya Habari na Wizara ya Nchi, Ofisi ya Rais, Maendeleo ya Vijana, zishirikiane na wadau wa sekta ya teknolojia ili vijana wapate manufaa hayo.

Dkt Samia ameyasema hayo leo, Ijumaa Aprili 10, 2026 jijini Dodoma, wakati wa uzinduzi huo, ukiambatana na kuunganisha huduma za mkongo wa Taifa wa mawasiliano katika Wilaya 85.

“Uwekezaji huu kwa vijana ni muhimu kwa sababu dunia ya teknolojia ni ya kwao. Dunia hii ipo viganjani mwao na ndiyo mfumo wa maisha yao. Ni lazima tuwawezeshe na kuwahamasisha kutumia mifumo hii ili waweze kukua kiuchumi na kijamii,” amesema.

Continue Reading

News

Dkt Samia azindua minara 758, kuwanufaisha zaidi ya wananchi milioni nane

Published

on

By

Na Mwandishi wetu, News info

Zaidi ya wananchi milioni 8.5 hususan wanaoishi mipakani na vijijini, wanatarajiwa kuondolewa changamoto ya mtandao, baada ya Rais Dkt Samia Suluhu Hassan, kuzindua minara 758 ya mawasiliano iliyojengwa katika maeneo mbalimbali nchini.

Uzinduzi huo umefanyika leo Ijumaa Aprili 10, 2026 jijini Dodoma, ukiambatana na kuunganisha huduma za mkongo wa Taifa wa mawasiliano katika Wilaya 85, ikiwa ni juhudi za Serikali kuimarisha uchumi wa kidijitali na kuongeza huduma za mawasiliano.

Akizungumza wakati wa uzinduzi huo, Dkt Samia amesema uwekezaji huo umetokana na ushirikiano kati ya Serikali na wadau wa sekta ya mawasiliano ili kuhakikisha huduma za mawasiliano zinawafikia wananchi kwa ubora unaokidhi mahitaji ya teknolojia ya kisasa na kwa gharama nafuu.

Amesema kukamilika kwa ujenzi wa minara hiyo kutachochea ushiriki wa wananchi katika uchumi wa kidijitali na kufungua fursa mpya za ajira, kuboresha utoaji wa huduma za kijamii na kuharakisha maendeleo ya Taifa.

“Mawasiliano si tena huduma ya anasa kama ilivyokuwa zamani. Leo hii ni uti wa mgongo wa uchumi wa kisasa na daraja la fursa kwa wananchi katika nyanja mbalimbali za maendeleo,” amesema

Continue Reading

Trending

Copyright © 2025 Newsinfo.