Connect with us

News

Kwanini Serikali inashirikiana na sekta binafsi

Published

on

Na Mwandishi wetu, News Info Online

Dar es Salaam. Ofisi ya Msajili wa Hazina (OMH) leo, Machi 5, 2026, imesema Serikali iliamua kushirikiana na sekta binafsi katika uendeshaji wa baadhi ya mashirika ili kuongeza ufanisi, mtaji na matumizi ya teknolojia katika kuendeleza uchumi wa nchi.

Mkurugenzi wa Usimamizi wa Utendaji, Ufuatiliaji na Tathmini ya Mashirika ya Kibiashara kutoka OMH, Lightness Mauki, alisema ushirikiano huo ni sehemu ya mkakati wa Serikali wa kuimarisha ufanisi wa mashirika pamoja na kuvutia uwekezaji.

Bi. Mauki alitoa kauli hiyo wakati akizungumza katika kipindi cha Kumekucha kinachorushwa na ITV Tanzania, ikiwa ni sehemu ya maandalizi kuelekea mkutano wa Wakurugenzi wa Bodi za kampuni ambazo Serikali ina umiliki wa hisa chache, unaotarajiwa kufanyika Machi 16 hadi 18 mwaka huu katika ukumbi wa PAPU Tower, Arusha.

Akifafanua historia ya uamuzi wa Serikali kushirikiana na sekta binafsi, alisema miaka ya nyuma Serikali ilikuwa na zaidi ya mashirika ya umma 400, lakini baadaye iliamua kuuza baadhi yake kwa sekta binafsi na kubaki na machache ambayo inamiliki hisa chache.

“Yalikuwa zaidi ya mashirika 400. Tuliamua kuuza baadhi kwa sekta binafsi na kubaki na kampuni 56 ambazo tuna hisa chache,” alisema Bi. Mauki.

Aliongeza: Tuli ‘offload’ hisa ili sekta binafsi ichukue hisa nyingi zaidi, hatua ambayo inatuwezesha kushirikiana katika ujuzi, mtaji na teknolojia na kuhakikisha kampuni hizo ziendelee kukua.”

Aidha, ushirikiano huo una manufaa kwa pande zote mbili: sekta binafsi inapata fursa ya kuwekeza na kupata faida, huku Serikali ikipata gawio na kuhakikisha uwekezaji unawanufaisha wananchi.

Katika kipindi cha miaka mitano iliyopita, gawio kutoka kwa kampuni ambazo Serikali ina hisa chache limeongezeka kwa asilimia 357, kutoka Sh58.26 bilioni mwaka 2020 hadi kufikia Sh266.52 bilioni mwaka 2024, ikionesha ukuaji mkubwa na mafanikio ya mkakati wa kushirikiana na sekta binafsi.

Bi. Mauki alisema kuwa katika kipindi hicho hicho, uwekezaji wa Serikali katika kampuni ambazo inamiliki hisa chache uliongezeka kwa asilimia 140, ukipanda kutoka Sh1.5 trilioni hadi Sh3.6 trilioni, jambo linaloashiria ukuaji endelevu na ufanisi wa mkakati wa kushirikiana na sekta binafsi.

Akijibu swali la mtangazaji kuhusu nani anaweka nia ya kushirikiana na sekta binafsi katika uwekezaji wa kampuni hizo, Bi. Mauki alisema hatua hiyo ilikuwa ni mkakati wa Serikali wenye lengo la kuimarisha ufanisi katika mashirika ya umma.

“Serikali iliona mashirika ni mengi na wakati huo huo teknolojia inakua kwa kasi na mahitaji ya mtaji ni makubwa, hivyo kulikuwa na haja ya kufanya kazi na sekta binafsi ili tuweze kushirikiana katika uendeshaji wa mashirika hayo,” alisema.

Alifafanua kuwa mkakati huo ulilenga kuhakikisha Serikali inaendelea kubaki na hisa katika kampuni za kimkakati huku ikitoa nafasi kwa sekta binafsi kushiriki katika uwekezaji.

“Ulikuwa ni mkakati mahususi wa Serikali kuhakikisha tunagawanya hisa na tunabaki nazo chache kwenye mashirika na kampuni za kimkakati,” alisema.

Aliongeza kuwa Serikali haiwezi kuacha umiliki wote kwa sababu ina wajibu kwa umma.

“Huwezi kutoa asilimia 100 kwa sababu Serikali ina wajibu kwa umma kuhakikisha wananchi wanapata huduma na bidhaa mbalimbali,” alisema.

Kuhusu ushiriki wa vijana katika uwekezaji huo, Bi. Mauki alisema Serikali imeandaa mkakati mpya kupitia Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 pamoja na mpango wa muda mrefu wa miaka 25 wa OMH utakaonza kutumika Julai 1, 2026.

Alisema mpango huo utapanua wigo wa kampuni na taasisi zitakazoingizwa kwenye soko la hisa ili kuwapa wananchi wengi zaidi, hususan vijana, nafasi ya kumiliki hisa na kupata gawio.

“Kuna mkakati ambao tumeuweka kupitia Dira ya Taifa 2050 pamoja na mpango wetu wa miaka 25 ambao utaanza Julai 1, 2025. Tutapanua wigo wa kampuni na taasisi tunazozileta kwenye soko la hisa pamoja na kuongeza ushiriki wa vijana,” alisema.

Aliongeza kuwa eneo la ushiriki wa vijana halikuguswa kwa kiwango kikubwa katika mpango unaoisha Juni 30 mwaka huu, lakini katika mpango mpya wa muda mrefu litapewa kipaumbele zaidi.

Continue Reading
Click to comment
0 0 votes
Article Rating
Subscribe
Notify of
guest
0 Comments
Oldest
Newest Most Voted
Inline Feedbacks
View all comments

News

Wanawake 142 waanza mafunzo ya Female Future Programme Dar es Salaam

Published

on

By

Na Mwandishi wetu, News info

Zaidi ya wanawake 142 wamepokelewa rasmi kushiriki toleo la 12 la programu ya mafunzo ya uongozi kwa wanawake, Female Future Programme (FFP), iliyofanyika jijini Dar es Salaam.

Mafunzo hayo ya kiutendaji yameandaliwa na Chama cha Waajiri Tanzania (ATE) kwa kushirikiana na Taasisi ya Usimamizi ya Afrika Mashariki na Kusini (ESAMI).

Mkurugenzi Mtendaji wa ATE, Bi. Suzanne Ndomba-Doran amesema programu hiyo imekuwa na mchango mkubwa kwa zaidi ya wanawake 800 waliokwisha pata mafunzo kwa zaidi ya muongo mmoja, na sasa inaendeshwa katika nchi sita kwa ufadhili wa NHO, huku akiwahamasisha washiriki kushiriki kikamilifu safari ya miezi tisa ya mafunzo. Aidha, Naibu Mkurugenzi Mkuu wa ESAMI, Dkt. David Kalaba amesema jamii inahitaji wanawake viongozi wenye kujiamini na uwezo mkubwa katika kipindi hiki cha mabadiliko ya haraka, akisisitiza umuhimu wa mtazamo wa kimataifa, kujifunza na kuendana na mabadiliko pamoja na uwezo wa kusimamia utofauti, kutatua migogoro na kutoa thamani kwa wateja.

Kwa upande wake, Meneja wa Upstream wa IFC, Bw. Sam Nganga aliyemwakilisha Meneja wa Nchi, Bi. Martine Valcin amesema taasisi hiyo inaendelea kuhakikisha wanawake wanapewa nafasi katika ngazi za juu za uongozi ili kukuza ushirikishwaji, huku akiwahimiza washiriki kujisimamia na kutumia kikamilifu mafunzo hayo.

Katika hafla hiyo pia kulikuwa na mjadala wa jopo kuhusu wanawake katika uongozi uliowashirikisha wataalamu mbalimbali wa rasilimali watu na uongozi kutoka taasisi tofauti, ambapo ilisisitizwa kuwa kuchanganya uzoefu wa vizazi tofauti vya wanawake kazini huleta matokeo chanya pamoja na umuhimu wa kujifunza ujuzi mpya na kuimarisha mentorship baada ya mafunzo.

Washiriki wa kundi la 12 walihimizwa kujenga mitandao imara ya kitaaluma, huku taasisi na makampuni yakitakiwa kutambua upekee wa kila mwanamke badala ya kuwaona kama kundi moja.

Akihitimisha, Mjumbe wa Bodi ya ATE, Bw. Gasper Kikui amesema sekta isiyo rasmi bado ina changamoto nyingi za uongozi na kuwataka washiriki kuyachukulia mafunzo hayo kwa uzito ili kuleta mabadiliko chanya.

Continue Reading

News

Dkt Samia: Vijana wanufaike na uwekezaji katika mawasiliano

Published

on

By

Na Mwandishi wetu, News info

Rais Dkt Samia Suluhu Hassan, ametaka vijana wanufaike ipasavyo na huduma za mkongo wa Taifa wa mawasiliano, hasa katika maeneo ya kukuza ubunifu, ujuzi wa kidigitali na fursa za ajira.

Ametaka Wizara ya Mawasiliano na Teknolojia ya Habari na Wizara ya Nchi, Ofisi ya Rais, Maendeleo ya Vijana, zishirikiane na wadau wa sekta ya teknolojia ili vijana wapate manufaa hayo.

Dkt Samia ameyasema hayo leo, Ijumaa Aprili 10, 2026 jijini Dodoma, wakati wa uzinduzi huo, ukiambatana na kuunganisha huduma za mkongo wa Taifa wa mawasiliano katika Wilaya 85.

“Uwekezaji huu kwa vijana ni muhimu kwa sababu dunia ya teknolojia ni ya kwao. Dunia hii ipo viganjani mwao na ndiyo mfumo wa maisha yao. Ni lazima tuwawezeshe na kuwahamasisha kutumia mifumo hii ili waweze kukua kiuchumi na kijamii,” amesema.

Continue Reading

News

Dkt Samia azindua minara 758, kuwanufaisha zaidi ya wananchi milioni nane

Published

on

By

Na Mwandishi wetu, News info

Zaidi ya wananchi milioni 8.5 hususan wanaoishi mipakani na vijijini, wanatarajiwa kuondolewa changamoto ya mtandao, baada ya Rais Dkt Samia Suluhu Hassan, kuzindua minara 758 ya mawasiliano iliyojengwa katika maeneo mbalimbali nchini.

Uzinduzi huo umefanyika leo Ijumaa Aprili 10, 2026 jijini Dodoma, ukiambatana na kuunganisha huduma za mkongo wa Taifa wa mawasiliano katika Wilaya 85, ikiwa ni juhudi za Serikali kuimarisha uchumi wa kidijitali na kuongeza huduma za mawasiliano.

Akizungumza wakati wa uzinduzi huo, Dkt Samia amesema uwekezaji huo umetokana na ushirikiano kati ya Serikali na wadau wa sekta ya mawasiliano ili kuhakikisha huduma za mawasiliano zinawafikia wananchi kwa ubora unaokidhi mahitaji ya teknolojia ya kisasa na kwa gharama nafuu.

Amesema kukamilika kwa ujenzi wa minara hiyo kutachochea ushiriki wa wananchi katika uchumi wa kidijitali na kufungua fursa mpya za ajira, kuboresha utoaji wa huduma za kijamii na kuharakisha maendeleo ya Taifa.

“Mawasiliano si tena huduma ya anasa kama ilivyokuwa zamani. Leo hii ni uti wa mgongo wa uchumi wa kisasa na daraja la fursa kwa wananchi katika nyanja mbalimbali za maendeleo,” amesema

Continue Reading

Trending

Copyright © 2025 Newsinfo.