Connect with us

News

Ofisi ya Msajili wa Hazina yahitimisha semina ya siku tano kwa kamati za bungeNa Mwandishi wa OMH

Published

on

Na Mwandishi wetu, News Info Online

Dodoma. Ofisi ya Msajili wa Hazina (OMH) imehitimisha semina ya siku tano kwa Kamati za Kudumu za Bunge za Uwekezaji wa Mitaji ya Umma (PIC) na ile ya Hesabu za Serikali (PAC), iliyofanyika kuanzia Februari 9 hadi 13, 2026, ikiwa ni mwendelezo wa mkakati wa kujenga uwezo wa Waheshimiwa Wabunge katika eneo la usimamizi na tathmini ya uwekezaji wa Serikali.

Kwa kipindi chote cha semina, OMH imewasilisha mada za kimkakati zilizolenga kuimarisha uelewa wa Kamati kuhusu nafasi ya Ofisi katika kuhifadhi, kusimamia na kuongeza thamani ya mitaji ya umma.

Mafunzo haya yalijikita katika kuoanisha wajibu wa kikatiba wa Kamati za PIC, PAC na jukumu la kisheria la OMH chini ya Sheria ya Msajili wa Hazina, Sura 370, ili kuhakikisha kuna uelewa wa pamoja kuhusu mifumo ya usimamizi, tathmini na uwajibikaji.

Katika mada ya ufanisi wa mitaji ya umma kupitia uanzishaji, uendelezaji na usimamizi wa kampuni tanzu, OMH ilieleza misingi ya kisheria na kiutendaji inayotumika kuanzisha kampuni hizo, kuanzia upembuzi yakinifu, idhini za mamlaka husika, hadi mifumo ya uendeshaji na tathmini.

Ilisisitizwa kuwa kampuni tanzu zimekuwa nyenzo ya kimkakati katika kukuza sekta za nishati, maji, kilimo na uchukuzi, kuongeza mapato yasiyo ya kodi na kupunguza utegemezi wa bajeti kuu ya Serikali.

Kwa upande wa mada kuhusu uainishaji na usimamizi wa mashirika ya umma kwa mujibu wa umiliki wa hisa, OMH iliwasilisha takwimu zinazoonesha kuwa inasimamia taasisi, mashirika na kampuni 308, zikiwemo 252 zinazomilikiwa na Serikali na 56 ambazo Serikali ina hisa chache.

Kamati zilielezwa mifumo tofauti ya usimamizi kwa mashirika ya umiliki mkubwa na yale ya ubia, pamoja na namna tathmini ya utendaji inavyofanyika kwa kuzingatia matokeo ya kifedha, ubora wa huduma, utawala bora na mchango wa kiuchumi.

Katika kipindi cha miaka mitano iliyopita, uwekezaji wa Serikali umeongezeka kutoka Sh67 trilioni hadi Sh92.3 trilioni, huku mapato yasiyo ya kodi yakiongezeka kutoka Sh637 bilioni hadi Sh1.028 trilioni.

Takwimu hizi ziliwasilishwa kama kiashiria cha kuimarika kwa usimamizi wa mitaji ya umma na mageuzi yanayoendelea ndani ya mashirika.

Aidha, semina ilijumuisha mada mahsusi kuhusu matumizi ya Mpango Mkakati, Mpango wa Uwekezaji na Mpango wa Biashara katika kutathmini ufanisi wa uwekezaji.

OMH ilieleza kuwa nyaraka hizi tatu ndizo msingi wa upangaji, utekelezaji na tathmini ya shughuli za taasisi na mashirika ya umma.

Mpango Mkakati wa miaka mitano huweka dira, dhamira, malengo ya kimkakati na viashiria vya kupima mafanikio.

Mpango wa Uwekezaji hubainisha miradi ya kipaumbele, tathmini za uwezekano na vyanzo vya fedha, wakati Mpango wa Biashara hutafsiri malengo ya kimkakati kuwa shughuli za kila mwaka na bajeti za utekelezaji.

Ilifafanuliwa kuwa mipango hii hufanya kazi kama mfumo mmoja uliounganishwa. Mpango Mkakati hutoa mwelekeo wa muda mrefu, Mpango wa Uwekezaji huainisha miradi itakayotekeleza mwelekeo huo, na Mpango wa Biashara huongoza utekelezaji wa kila siku.

Kupitia mfumo huu, OMH hutathmini kama rasilimali za umma zinawekezwa kwa kuzingatia thamani halisi ya fedha.

Kwa mfano, katika mashirika ya miundombinu, utekelezaji wa miradi hupimwa kwa kuoanisha ratiba, bajeti na matokeo yaliyotarajiwa.

Katika mashirika ya kifedha ambako Serikali ina hisa, tathmini huzingatia gawio, thamani ya hisa na mchango katika Mfuko Mkuu wa Serikali.

Aidha, OMH hutumia viashiria vya utendaji (KPIs) vilivyomo kwenye Mipango Mkakati kupima ROI, uendelevu wa kifedha na mchango wa kiuchumi.

Semina pia ilijadili maeneo yanayohitaji maboresho, ikiwemo kutooanishwa kwa baadhi ya mipango, udhaifu wa viashiria visivyopimika na ucheleweshaji wa taarifa za utendaji.

Katika kukabiliana na changamoto hizo, OMH imeanza kuimarisha mikataba ya utendaji kwa kutumia washauri elekezi kuanzia mwaka wa fedha 2025/26, kuanzisha mfumo wa kidijitali wa ufuatiliaji wa mipango kwa kushirikiana na Tume ya Taifa ya Mipango, pamoja na kuendeleza maboresho ya mwongozo wa usimamizi wa uwekezaji wa umma (Public Investment Management – PIM).

Kwa ujumla, semina ya siku tano imeonesha ushirikiano wa karibu kati ya OMH na Kamati ya PIC katika kuimarisha uwazi, uwajibikaji na ufanisi wa usimamizi wa mitaji ya umma.

OMH imeweka wazi kuwa itaendelea kutoa taarifa, mafunzo na ushauri wa kitaalamu kwa Bunge ili kuhakikisha uwekezaji wa Serikali unaleta thamani endelevu kwa uchumi wa Taifa na kwa wananchi.

Continue Reading
Click to comment
0 0 votes
Article Rating
Subscribe
Notify of
guest
0 Comments
Oldest
Newest Most Voted
Inline Feedbacks
View all comments

News

Wanawake 142 waanza mafunzo ya Female Future Programme Dar es Salaam

Published

on

By

Na Mwandishi wetu, News info

Zaidi ya wanawake 142 wamepokelewa rasmi kushiriki toleo la 12 la programu ya mafunzo ya uongozi kwa wanawake, Female Future Programme (FFP), iliyofanyika jijini Dar es Salaam.

Mafunzo hayo ya kiutendaji yameandaliwa na Chama cha Waajiri Tanzania (ATE) kwa kushirikiana na Taasisi ya Usimamizi ya Afrika Mashariki na Kusini (ESAMI).

Mkurugenzi Mtendaji wa ATE, Bi. Suzanne Ndomba-Doran amesema programu hiyo imekuwa na mchango mkubwa kwa zaidi ya wanawake 800 waliokwisha pata mafunzo kwa zaidi ya muongo mmoja, na sasa inaendeshwa katika nchi sita kwa ufadhili wa NHO, huku akiwahamasisha washiriki kushiriki kikamilifu safari ya miezi tisa ya mafunzo. Aidha, Naibu Mkurugenzi Mkuu wa ESAMI, Dkt. David Kalaba amesema jamii inahitaji wanawake viongozi wenye kujiamini na uwezo mkubwa katika kipindi hiki cha mabadiliko ya haraka, akisisitiza umuhimu wa mtazamo wa kimataifa, kujifunza na kuendana na mabadiliko pamoja na uwezo wa kusimamia utofauti, kutatua migogoro na kutoa thamani kwa wateja.

Kwa upande wake, Meneja wa Upstream wa IFC, Bw. Sam Nganga aliyemwakilisha Meneja wa Nchi, Bi. Martine Valcin amesema taasisi hiyo inaendelea kuhakikisha wanawake wanapewa nafasi katika ngazi za juu za uongozi ili kukuza ushirikishwaji, huku akiwahimiza washiriki kujisimamia na kutumia kikamilifu mafunzo hayo.

Katika hafla hiyo pia kulikuwa na mjadala wa jopo kuhusu wanawake katika uongozi uliowashirikisha wataalamu mbalimbali wa rasilimali watu na uongozi kutoka taasisi tofauti, ambapo ilisisitizwa kuwa kuchanganya uzoefu wa vizazi tofauti vya wanawake kazini huleta matokeo chanya pamoja na umuhimu wa kujifunza ujuzi mpya na kuimarisha mentorship baada ya mafunzo.

Washiriki wa kundi la 12 walihimizwa kujenga mitandao imara ya kitaaluma, huku taasisi na makampuni yakitakiwa kutambua upekee wa kila mwanamke badala ya kuwaona kama kundi moja.

Akihitimisha, Mjumbe wa Bodi ya ATE, Bw. Gasper Kikui amesema sekta isiyo rasmi bado ina changamoto nyingi za uongozi na kuwataka washiriki kuyachukulia mafunzo hayo kwa uzito ili kuleta mabadiliko chanya.

Continue Reading

News

Dkt Samia: Vijana wanufaike na uwekezaji katika mawasiliano

Published

on

By

Na Mwandishi wetu, News info

Rais Dkt Samia Suluhu Hassan, ametaka vijana wanufaike ipasavyo na huduma za mkongo wa Taifa wa mawasiliano, hasa katika maeneo ya kukuza ubunifu, ujuzi wa kidigitali na fursa za ajira.

Ametaka Wizara ya Mawasiliano na Teknolojia ya Habari na Wizara ya Nchi, Ofisi ya Rais, Maendeleo ya Vijana, zishirikiane na wadau wa sekta ya teknolojia ili vijana wapate manufaa hayo.

Dkt Samia ameyasema hayo leo, Ijumaa Aprili 10, 2026 jijini Dodoma, wakati wa uzinduzi huo, ukiambatana na kuunganisha huduma za mkongo wa Taifa wa mawasiliano katika Wilaya 85.

“Uwekezaji huu kwa vijana ni muhimu kwa sababu dunia ya teknolojia ni ya kwao. Dunia hii ipo viganjani mwao na ndiyo mfumo wa maisha yao. Ni lazima tuwawezeshe na kuwahamasisha kutumia mifumo hii ili waweze kukua kiuchumi na kijamii,” amesema.

Continue Reading

News

Dkt Samia azindua minara 758, kuwanufaisha zaidi ya wananchi milioni nane

Published

on

By

Na Mwandishi wetu, News info

Zaidi ya wananchi milioni 8.5 hususan wanaoishi mipakani na vijijini, wanatarajiwa kuondolewa changamoto ya mtandao, baada ya Rais Dkt Samia Suluhu Hassan, kuzindua minara 758 ya mawasiliano iliyojengwa katika maeneo mbalimbali nchini.

Uzinduzi huo umefanyika leo Ijumaa Aprili 10, 2026 jijini Dodoma, ukiambatana na kuunganisha huduma za mkongo wa Taifa wa mawasiliano katika Wilaya 85, ikiwa ni juhudi za Serikali kuimarisha uchumi wa kidijitali na kuongeza huduma za mawasiliano.

Akizungumza wakati wa uzinduzi huo, Dkt Samia amesema uwekezaji huo umetokana na ushirikiano kati ya Serikali na wadau wa sekta ya mawasiliano ili kuhakikisha huduma za mawasiliano zinawafikia wananchi kwa ubora unaokidhi mahitaji ya teknolojia ya kisasa na kwa gharama nafuu.

Amesema kukamilika kwa ujenzi wa minara hiyo kutachochea ushiriki wa wananchi katika uchumi wa kidijitali na kufungua fursa mpya za ajira, kuboresha utoaji wa huduma za kijamii na kuharakisha maendeleo ya Taifa.

“Mawasiliano si tena huduma ya anasa kama ilivyokuwa zamani. Leo hii ni uti wa mgongo wa uchumi wa kisasa na daraja la fursa kwa wananchi katika nyanja mbalimbali za maendeleo,” amesema

Continue Reading

Trending

Copyright © 2025 Newsinfo.