Connect with us

News

NMB Yawatambua wanafunzi bora na Kuimarisha Ushirikiano na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam

Published

on

Na Mwandishi Wetu Maalum

Benki ya NMB kwa kushirikiana na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Kitivo cha Biashara, imewatambua wanafunzi kumi bora katika kozi kumi waliomaliza masomo mwaka huu kwa hafla maalum ya utoaji wa zawadi mbalimbali, ikiwatambua kwa mafanikio yao ya kitaaluma na juhudi kubwa iliyowaletea ufaulu.

Hafla iliyofanyika siku moja kabla ya kuanza kwa mahafali za chuo hicho, zawadi za pesa taslimu, vyeti na fursa za mafunzo kazini kwa washindi hao zilitolewa na Benki ya NMB huku wawakilishi wa Benki hiyo wakipongeza juhudi kubwa za wahitimu na chuo kwa ujumla katika dhamira yao ya kukuza vipaji na maendeleo ya kitaalamu.

Kwa niaba ya Benki ya NMB, Mgeni Rasmi wa shuguli hiyo, Mkuu wa Idara ya Rasilimali Watu, Kituo cha Utaalamu wa Benki ya NMB, Joanitha Mrengo, alielezea fahari ya Benki katika kuunga mkono juhudi mbalimbali za vijana na hususani za kitaaluma ambazo zitazaa watalaamu bora kwa maslahi ya taifa kwa ujumla.

“Kwetu sisi ni fahari kubwa kushiriki katika kutambua bidii na juhudi za vijana hawa wadogo, alisema joanitha.

“Leo hii tunashuhudia nidhamu, uvumilivu na ubora wao wa kitaaluma ukileta majibu stahiki. Benki ya NMB itatengeneza fursa kuanzia za ajira na hata za mafunzo kazini ambazo tunaamini zitawawezesha wataalamu hawa kustawi katika soko la ajira.”

Mrengo aliongeza kuwa Benki ya NMB inaendelea kujivunia ushirikiano wa dhati uliopo baina ya taasisi hiyo ya fedha na chuo kikuu cha dar es salaam kwani wameshafanya mengi ikiwemo kutoa fursa za kuwapa wanafunzi nafasi za kujifunza wakiwa masomoni katika benki hiyo na hivyo kuchangia katika kuzalisha wataalamu zaidi katika sekta ya kifedha.

“Mbali na mafunzo wakiwa kazini watakayopata washindi wetu wa leo, tumekuwa na ushirikiano na Chuo kikuu cha Dar es Salaam katika kuendelea kutoa mafunzo kwa vitendo kwa wanafunzi wa chuo hiki. Lakini pia tunayo makubaliano makubwa ya kuendelea kushirikiana katika masuala ya kitehama,” Alisema Mrengo.

Naye Naibu Makamu Mkuu wa Chuo, Utafiti, Profesa Nelson Boniface, pia alisisitiza umuhimu wa ushirikiano huo akisema, “Ushirikiano wetu na Benki ya NMB unaboresha ubora wa elimu tunayoitoa na unachangia kwa kiasi kikubwa katika maendeleo ya taifa. Pamoja, tunatengeneza viongozi watakaochochea maendeleo ya Tanzania.”

Naibu Makamu Mkuu pia alibainisha kwamba Chuo Kikuu cha Dar es Salaam kitatumia wataalamu mbalimbali ikiwemo wale wa NMB kutoa mihadhara maalum, ili kuwapa wanafunzi maarifa ya vitendo katika nyanja zao.

Jitihada hizi zikilenga kuwapa wanafunzi elimu ya kitaaluma pamoja na maarifa halisi ya kazi, kuwapa wanafunzi mtazamo mpana zaidi nje ya darasa na kuwaandaa vyema kwa changamoto zijazo.

Mkuu wa Idara ya Wanafunzi wa Chuo, Profesa Omary Mbura, alielezea nafasi ya NMB kama mshirika wa kina: “Benki ya NMB imekuwa ikituunga mkono si tu kwa msaada wa kifedha bali pia kwa kushiriki kikamilifu katika miradi yetu ya kitaaluma na jamii,” alisema.

Ushirikiano kati ya Benki ya NMB na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam unaakisi dhamira ya pamoja ya ubora, ubunifu na ukuaji kwa Taifa.

Wakati chuo kinaendelea kulea viongozi wa kesho, ushirikiano huu ni hatua ya kimkakati kuelekea kuleta mafanikio makubwa ya kitaaluma na yenye tija kwa taifa kwa ujumla.

Akizungumza wakati wa hafla hiyo, Meneja wa Benki ya NMB kanda ya Dar es Salaam, Seka Urio alisema, “Tunatarajia kuimarisha zaidi uhusiano huu, ambao unawanufaisha si tu wanafunzi na wafanyakazi wa chuo bali pia unachangia katika maendeleo ya uchumi wetu na kwa pamoja, tunajenga mustakabali mzuri wa Tanzania.”

Continue Reading
Click to comment
0 0 votes
Article Rating
Subscribe
Notify of
guest
0 Comments
Oldest
Newest Most Voted
Inline Feedbacks
View all comments

News

Wanawake 142 waanza mafunzo ya Female Future Programme Dar es Salaam

Published

on

By

Na Mwandishi wetu, News info

Zaidi ya wanawake 142 wamepokelewa rasmi kushiriki toleo la 12 la programu ya mafunzo ya uongozi kwa wanawake, Female Future Programme (FFP), iliyofanyika jijini Dar es Salaam.

Mafunzo hayo ya kiutendaji yameandaliwa na Chama cha Waajiri Tanzania (ATE) kwa kushirikiana na Taasisi ya Usimamizi ya Afrika Mashariki na Kusini (ESAMI).

Mkurugenzi Mtendaji wa ATE, Bi. Suzanne Ndomba-Doran amesema programu hiyo imekuwa na mchango mkubwa kwa zaidi ya wanawake 800 waliokwisha pata mafunzo kwa zaidi ya muongo mmoja, na sasa inaendeshwa katika nchi sita kwa ufadhili wa NHO, huku akiwahamasisha washiriki kushiriki kikamilifu safari ya miezi tisa ya mafunzo. Aidha, Naibu Mkurugenzi Mkuu wa ESAMI, Dkt. David Kalaba amesema jamii inahitaji wanawake viongozi wenye kujiamini na uwezo mkubwa katika kipindi hiki cha mabadiliko ya haraka, akisisitiza umuhimu wa mtazamo wa kimataifa, kujifunza na kuendana na mabadiliko pamoja na uwezo wa kusimamia utofauti, kutatua migogoro na kutoa thamani kwa wateja.

Kwa upande wake, Meneja wa Upstream wa IFC, Bw. Sam Nganga aliyemwakilisha Meneja wa Nchi, Bi. Martine Valcin amesema taasisi hiyo inaendelea kuhakikisha wanawake wanapewa nafasi katika ngazi za juu za uongozi ili kukuza ushirikishwaji, huku akiwahimiza washiriki kujisimamia na kutumia kikamilifu mafunzo hayo.

Katika hafla hiyo pia kulikuwa na mjadala wa jopo kuhusu wanawake katika uongozi uliowashirikisha wataalamu mbalimbali wa rasilimali watu na uongozi kutoka taasisi tofauti, ambapo ilisisitizwa kuwa kuchanganya uzoefu wa vizazi tofauti vya wanawake kazini huleta matokeo chanya pamoja na umuhimu wa kujifunza ujuzi mpya na kuimarisha mentorship baada ya mafunzo.

Washiriki wa kundi la 12 walihimizwa kujenga mitandao imara ya kitaaluma, huku taasisi na makampuni yakitakiwa kutambua upekee wa kila mwanamke badala ya kuwaona kama kundi moja.

Akihitimisha, Mjumbe wa Bodi ya ATE, Bw. Gasper Kikui amesema sekta isiyo rasmi bado ina changamoto nyingi za uongozi na kuwataka washiriki kuyachukulia mafunzo hayo kwa uzito ili kuleta mabadiliko chanya.

Continue Reading

News

Dkt Samia: Vijana wanufaike na uwekezaji katika mawasiliano

Published

on

By

Na Mwandishi wetu, News info

Rais Dkt Samia Suluhu Hassan, ametaka vijana wanufaike ipasavyo na huduma za mkongo wa Taifa wa mawasiliano, hasa katika maeneo ya kukuza ubunifu, ujuzi wa kidigitali na fursa za ajira.

Ametaka Wizara ya Mawasiliano na Teknolojia ya Habari na Wizara ya Nchi, Ofisi ya Rais, Maendeleo ya Vijana, zishirikiane na wadau wa sekta ya teknolojia ili vijana wapate manufaa hayo.

Dkt Samia ameyasema hayo leo, Ijumaa Aprili 10, 2026 jijini Dodoma, wakati wa uzinduzi huo, ukiambatana na kuunganisha huduma za mkongo wa Taifa wa mawasiliano katika Wilaya 85.

“Uwekezaji huu kwa vijana ni muhimu kwa sababu dunia ya teknolojia ni ya kwao. Dunia hii ipo viganjani mwao na ndiyo mfumo wa maisha yao. Ni lazima tuwawezeshe na kuwahamasisha kutumia mifumo hii ili waweze kukua kiuchumi na kijamii,” amesema.

Continue Reading

News

Dkt Samia azindua minara 758, kuwanufaisha zaidi ya wananchi milioni nane

Published

on

By

Na Mwandishi wetu, News info

Zaidi ya wananchi milioni 8.5 hususan wanaoishi mipakani na vijijini, wanatarajiwa kuondolewa changamoto ya mtandao, baada ya Rais Dkt Samia Suluhu Hassan, kuzindua minara 758 ya mawasiliano iliyojengwa katika maeneo mbalimbali nchini.

Uzinduzi huo umefanyika leo Ijumaa Aprili 10, 2026 jijini Dodoma, ukiambatana na kuunganisha huduma za mkongo wa Taifa wa mawasiliano katika Wilaya 85, ikiwa ni juhudi za Serikali kuimarisha uchumi wa kidijitali na kuongeza huduma za mawasiliano.

Akizungumza wakati wa uzinduzi huo, Dkt Samia amesema uwekezaji huo umetokana na ushirikiano kati ya Serikali na wadau wa sekta ya mawasiliano ili kuhakikisha huduma za mawasiliano zinawafikia wananchi kwa ubora unaokidhi mahitaji ya teknolojia ya kisasa na kwa gharama nafuu.

Amesema kukamilika kwa ujenzi wa minara hiyo kutachochea ushiriki wa wananchi katika uchumi wa kidijitali na kufungua fursa mpya za ajira, kuboresha utoaji wa huduma za kijamii na kuharakisha maendeleo ya Taifa.

“Mawasiliano si tena huduma ya anasa kama ilivyokuwa zamani. Leo hii ni uti wa mgongo wa uchumi wa kisasa na daraja la fursa kwa wananchi katika nyanja mbalimbali za maendeleo,” amesema

Continue Reading

Trending

Copyright © 2025 Newsinfo.